Wednesday 22 February 2017

HALMASHAURI NCHINI ZASHAURIWA KUACHANA NA MFUMO WA KUTUMIA WAZABUNI KATIKA KUKUSANYA USHURU MDOGOMDOGO.

Na: Frank Shija - MAELEZO
Halmashauri nchini zimeshauriwa kupunguza mlolongo katika mchakato wa ukusanyaji wa ushuru mdogomdogo unaotokana na kutumia mfumo wa kutumia wazabuni  badala yake kazi hiyo ifanywe na watendaji wa Halmashauri husika.

Ushauri huo umetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) George Boniphace Simbachawene katika mahojiano na mtangazaji wa Kituo cha luninga cha ITV kupitia kipindi cha Dakika 45 hivi karibuni.

Simbachawene alisema kuwa kumekuwa na kasumba ya Halmashauri nchini kutumia wazabuni katika ukusanyaji wa ushuru jambo linalochangia kusababisha mianya ya ubadhirifu wa fedha za umma.

“Mawakala wa ukusanyaji ushuru wamekuwa wadanganyifu na mara zingine wamekuwa wakiwasumbua wafanyabiashara ni vyema sasa Halmashauri nchini zikafikiria kutumia watendaji wake katika zoezi zima la ukusanyaji ushuru,” alisema Simbachawene.

Aliongeza kuwa sambamba na ukusanyaji wa ushuru kufanywa na watendaji wa Halmashauri husika aliagiza fedha hizo kuhifadhiwa katika akaunti za halmashauri hizo.

Katika hatua nyingine Waziri Simbachawene amewapongeza watumishi wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kwa utendaji wao ambapo amesema umeanza kutia faraja.


Hata hivyo alitoa rai kwa watumishi hao kuendelea kubadilika na anayeona hawezi kuendana na kasi ya Serikali ya Awamu ya Tano ni vyema akapisha ili Watanzania wengine waweze kuajiriwa.

No comments:

Post a Comment