Pichani Luteni
Kanali Joseph Bakari (kushoto) akimkabidhi Katibu Mkuu wa Baraza hilo Kanali
Dorah Mamby Koita zawadi maalum (plaque) kwa niaba ya Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi
Jenerali Davis A. Mwamunyange alipowasili rasmi katika Sekretarieti ya Baraza
hilo.
Pichani Kanali
Bakari akiwa Meja akivisha Nishani na aliyekuwa Rais wa Baraza hilo Meja Jenerali Gianni Gola (Italia) kwa
kutambua mchango wake katika michezo huko Suriname Paramaribo Amerika ya kusini
mwaka 2008.
Waamuzi vijana
katika Kituo cha kukuza na kuendeleza michezo cha Twalipo Youth Sports
Foundation katika mazoezi.
...................................................................................................................
Sekretarieti ya Baraza la Michezo ya Majeshi Duniani (Conseil
International du Sport Militaire/International Military Sports Council
-CISM),yenye Makao yake makuu Jijini Brussels Nchini Ubelgiji, imepata nguvu
mpya baada ya Mtanzania Luteni Kanali Joseph Peter Bakari wa Jeshi la Ulinzi la
Wananchi wa Tanzania (JWTZ), kuteuliwa kushikizwa kwenye Sekretarieti ya Baraza
hilo kama Mshauri/ Msaidizi wa Mkurugenzi
wa Idara ya Michezo ya Baraza hilo (Advisor/ Special Assistant to the CISM
Sports Director). Katika utekelezaji wa majukumu yake Kanali Bakari anakuwa chini ya Mkurugenzi Kanali Carlos Eduardo kutoka Brazil.
Akiongea siku ya kumkaribisha rasmi, Katibu Mkuu wa Baraza hilo Kanali
Dorah Mamby Koita kutoka Guinea alisema” Sekretarieti imepokea kwa furaha
uteuzi na hatimaye ujio wa Kanali Bakari, kwani binafsi anamfahamu katika
utendaji wake kazi hususani kuendeleza na kukuza vipaji vya watoto katika
michezo, (Mwaka 2008 nchini Suriname Paramaribo Bodi ya wakurugenzi ya Baraza
hili ilimtunikia Nishani (CISM
Order of Merit) iitwayo The Grand Knight
kwa kutambua moyo wa kujitolewa, bidii, uaminifu na uadilifu katika kuenenda
sambamba na malengo ya CISM katika kuendeleza michezo.) Hivyo ni dhahiri kuwa atakuwa msaada
mkubwa katika Baraza hilo Kimataifa”.
Aliongeza kuwa Tanzania imefanya vyema kumshikiza Kanali Bakari kwani
hapa ataongeza uzoefu zaidi ambao
atautumia katika kuendeleza tasnia ya michezo Jeshini na kwa Taifa kwa ujumla
kutokana na ukweli kuwa Sekretarieti hiyo inaundwa na maafisa wenye uzoefu na
taaluma za hali ya juu katika tasnia ya michezo, utimamu wa mwili na viungo na
ambao wanatoka kwenye mataifa ambayo yamepiga hatua kubwa katika maendeleo ya
michezo kama vile Brazil, Ujerumani, Uhispania n.k”.
Akitoa neno la shukrani Kanali Bakari alisema kuwa amefarijika sana
kuwa miongoni mwa watendaji katika Baraza hilo. Aidha, alilishukuru JWTZ na
Taifa kwa ujumla kwa kumpa dhamana hiyo ya kimataifa. “ Kwa uwezo wa Mungu ,ni matarajio yangu kuwa
nitafanya kazi kwa weledi mkubwa na moyo
wa kujituma ili niweze kuitendea haki nafasi na fursa niliyopewa kwa manufaa ya
Baraza hilo, JWTZ na nchi yangu ya Tanzania kwa ujumla”.
Alisema.
Kanali Bakari ni muasisi wa program ya kukuza na kuendeleza vipaji
katika michezo ya Twalipo Youth Sports Foundation inayosimamiwa na JWTZ.
Programu hiyo pamoja na kuendeleza vipaji pia ni program ya kwanza nchini kutoa
mafunzo ya uamuzi katika mpira wa miguu. Waamuzi hao vijana kwa sasa wanatumika
kuchezesha mashindano mbalimbali hadi ngazi ya Ligi Kuu. Frank Domayo wa Azam
na Yohana Mkomola wa Serengeti Boys ni miongoni mwa matunda chanya ya programu
hiyo.
“CISM” ( International
Military Sports Council/ Baraza la Michezo ya Majeshi Duniani ni moja kati ya Shirikisho kubwa duniani
linalojishughulisha na michezo anuai (multdisplinary).Baraza hilo linaloundwa na majeshi ya nchi wanachama 134, Tanzania ikiwemo.
Dhima Kuu ya Shirikisho hilo ni kutumia michezo kama njia/zana ya
kueneza amani duniani badala ya vita. Hivyo kupitia Shirikisho hilo nchi
wanachama zinaaswa na kupewa wito kuwa
yale waliyokuwa wanayafanya katika uwanja wa vita sasa wayafanye katika viwanja
vya michezo.
Shirikisho hilo huandaa
mashindano mbalimbali ya michezo. Kwa mwaka huandaa zaidi ya mashindano 20 ya
dunia (World Championships), mashindano ya Mabara na kikanda katika michezo
zaidi ya 30. Masuala yahusiyo uongozi,
uamuzi, ualimu, tiba na katazo la
matumizi ya nguvu za kusisimua misuli katika michezo ni miongoni mwa mambo
muhimu yanayosimamiwa na shirikisho hilo.
Kanali Joseph Bakari anakuwa ni
Mtanzania wa Kwanza kuteuliwa katika sekretarieti ya Baraza hilo. Anajiunga na waafrika wengine
Kanali Dorah Mamby Koita kutoka Guinea na Kanali Abdulraheem Belo kutoka Nigeria.
Ni matarajio ya wapenda michezo kuwa Kanali Bakari atatoa uwakilishi
uliotukuka huko Brussels. Kila la heri!!!


