Na Mwamvua Mwinyi
MBUNGE wa jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete amepongeza jitihada kubwa zinazofanywa na wataaluma wa Halmashauri ya Chalinze katika kuboresha mradi wa maji wa Wami ambao utawezesha kuondoa kero ya maji jimboni hapo.
Akizungumza baada ya kutembelea mradi huo ,Ridhiwani alisema mradi huo ambao ulianzishwa na aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo Dkt Jakaya Kikwete ambae ni rais mstaafu wa awamu ya nne ni mmoja kati ya miradi bora iliyoleta ukombozi mkubwa wa upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi wa mji wa Chalinze .
Hivyo alisema lengo la kufanya ziara katika eneo la mradi huo ni kuona shughuli mbali mbali zinazofanywa na wataalam kwa ajili ya kuendelea kuboresha mradi huo ili kuwawezesha wananchi wake kupata huduma ya uhakika ya maji safi na salama .
" Mradi huu ni mkombozi mkubwa kwa wananchi wa jimbo la hili,nichukue fursa ya kuwapongeza wataalam wa halmashauri kwa kazi nzuri wanayoifanya ya uboreshaji wa mradi huu" alisema Ridhiwani.
Alieleza amefurahishwa na jitihada zinazoendelea kufanywa na wataalam wa Halmashauri hiyo kuhakikisha wananchi wanapata maji .
Ridhiwani alifafanua kazi yake akiwa ni mwakilishi wa wananchi ni kuendelea kuisimamia serikali kwa kuwawakilisha wananchi wake bungeni.
Ridhiwani aliwataka wananchi kuendelea kutunza miundo mbinu ya maji ili kuwezesha mradi huo kuendelea kuwa msaada kwao.
Mradi huo utakapokamilika utakuwa umetatua tatizo kubwa la ukosefu wa maji kwa wananchi hao.

0 Comments