Na Daudi Manongi-MAELEZO
........................
Serikali kupitia
Wakala wa Nishati Vijijini (REA),imeanza utekelezaji wa Mradi Kabambe wa Awamu
ya Tatu wa kusambaza nishati vijijini utakaojumuisha vijiji 7,873 katika wilaya
na mikoa yote ya Tanzania Bara ambao utatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano
(5) kuanzia mwaka huu wa fedha 2016/17 hadi 2020/21.
Hayo yamesemwa na
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Boniface Gissima Nyamo-Hanga katika Taarifa yake kwa vyombo vya
habari iliyotolewa leo Jijini Dar es Salaam.
Aidha Taarifa hiyo inasema kuwa vijiji 7697 vitapelekewa umeme wa gridi na vijiji 176 umeme wa nje ya gridi.
Utekelezaji wa Mradi
huu unajumuisha vipengele-mradi vitatu ambavyo
vimelenga kuongeza wigo wa miundombinu ya usambazaji umeme katika maeneo yenye
miundombinu ili kufikisha umeme kwenye vitongoji ambavyo havijafikiwa na umeme.Kipengele
kingine ni kufikisha umeme kwenye vijiji ambavyo havijafikiwa kabisa na
miundombinu ya umeme wa gridi na Kipengele cha tatu kinahusisha
uzalishaji na usambaji wa nishati jadidifu kwenye maeneo yaliyo mbali na
miundombinu ya umeme wa grid na kwenye visiwa.
Aidha Taarifa
hiyo inaeleza kuwa mradi huu umeanza na upo katika hatua mbalimbali ambapo kufuatia Mikataba iliyosainiwa
Mwezi Desemba 2016 katika mikoa sita ya Arusha, Iringa, Mara, Mbeya, Pwani, na
Tanga kwa gharama ya Dola za Marekani Milioni 27 kutoka Serikali ya Tanzania na
Norway, hivyo kuwezesha vijiji 305 kusambaziwa umeme.
Pia umeme utasambazwa kwenye vijiji 3,559 katika
mikoa 25 ya Tanzania Bara unaokadiriwa kugharimu Shilingi bilioni 733.98 kutoka
Serikali ya Tanzania, Norway, Sweden na Benki ya Dunia na utatekelezwa kwa
kipindi cha miezi 24 kuanzia mwaka wa fedha 2016/17 hadi 2017/18.
Taratibu za ununuzi zinaendelea na wakandarasi wataanza
kazi mwezi Aprili 2017 ambapo hadi sasa jumla ya vijiji 4,395 kati ya vijiji
12,268 ambayo ni sawa asilimia 36 vimeunganishwa na huduma ya umeme. Baada ya
kukamilika kwa mradi huu, jumla ya vijiji 7,934 sawa na asilimia 65 vitakuwa
vimefikiwa na umeme. Vijiji 4,334 vinavyosalia vitapelekewa umeme kuanzia mwaka
wa fedha 2018/19 hadi 2020/21 kutegemeana na upatikanaji wa fedha.
Kusambaza umeme kwenye vijiji 121 katika maeneo
yanayopitiwa na umeme wa Msongo wa Kilovoti 400 kutoka katika mikoa ya Iringa,
Dodoma, Singida, Tabora na Shinyanga kwa gharama ya dola za Marekani milioni 30
kwa ufadhili wa Serikali za Norway na Sweden. Taratibu za ununuzi wa
wakandarasi zinakamilishwa na utekelezaji utaanza mwezi Machi 2017.
Pamoja na hayo miradi ya umeme
wa nje ya Gridi inayotekelezwa na sekta binafsi imetengewa Jumla ya Dola za Marekani milioni
84 kwa ajili ya mradi huu ambapo kati ya hizo Dola za Marekani milioni 42
ni kutoka Serikali ya Uingereza na Dola za Marekani milioni 42 kutoka Benki ya
Dunia. Wakala ulitangaza awamu ya kwanza
ya mradi huu tarehe 23 Septemba, 2016 kwa ajili ya kushindanisha waendelezaji
binafsi na wajasiriamali wa nishati jadidifu kwenye maeneo ya nje ya gridi na
Awamu ya pili itatangazwa mwezi Aprili 2017, matangazo haya yatakuwa yanatolewa
kwa awamu kila baada miezi sita. Wajasirimali wa nishati jadidifu
wanahamasishwa kushiriki katika utekelezaji wa mradi huu.
Wakala unaishukuru Serikali kwa kuweka msisitizo kwenye
miradi ya usambazaji wa nishati bora vijijini pamoja na kuendelea kutoa fedha
kwa ajili ya utekelezaji wa miradi hiyo. Lengo la Serikali ni kufikisha umeme
kwenye vijiji vyote Tanzania Bara ifikapo Mwaka 2021; na kuongeza idadi ya
vijiji vilivyofikiwa na huduma ya umeme hadi asilimia 85 mwaka 2025 na asilimia
100 Mwaka 2030.

0 Comments