Subscribe Us

header ads

VIONGOZI WATAKIWA KUZINGATIA MAADILI NA MIIKO YA UONGOZI KATIKA UTENDAJI WAO

Na Nuru Juma na Husna Saidi - MAELEZO
Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu wa  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Benjamin William Mkapa amewataka viongozi wa nchi kuzingatia maadili na miiko ya uongozi ikiwa ni njia ya kumuenzi Hayati Baba wa Taifa Mwl. Julius Kambarage Nyerere.

Rai hiyo imetolewa leo wakati wa Kongamano la Maadhimisho ya Kumbukizi ya Mwl Nyerere lililofanyika  katika ukumbi wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwl. Nyerere Jijini Dar es Salaam.

Mkapa alisema kuwa katika kumuenzi Mwl. Nyerere ni vyema  viongozi wakamuenzi kwa kufuata maadili na miiko ya uongozi jambo litakalo pelekea kuwa viongozi bora katika jamii.

“Urithi wa Mwl. Nyerere katika uongozi ni kufuata yale aliyokuwa akiyafanya na katika uongozi wake aliweza kutekeleza na kuzingatia maadili na miiko ya uongozi kwa kuwaongoza wananchi kwa usawa na haki, hivyo  katika kumuenzi hatuna budi kufuata yale aliyoyafanya, ” alisema Mkapa.

Aidha Mkapa alitoa pongezi kwa uongozi wa chuo cha Kumbukumbu  ya Mwalimu Nyerere kwa kuweza kukiinua tena chuo hicho kwani kipindi cha kati chuo kililega na kupoteza mwelekeo.

Pia aliwataka Watanzania kuacha kubuni mambo wasiyoyajua na badala yake wapende sana kusoma na kuelewa historia ya nchi na Serikali kwa ujumla  ikiwa ni njia mojawapo ya kumuenzi baba wa Taifa.

“Napenda kuwasihi Watanzania wapende sana kusoma ili kuweza kutanua upeo wao wa kufikiri kwani Baba wa Taifa alipenda sana kusoma makala za ndani ya nchi, vitabu na makala za nje ya nchi ili kuweza kupanua upeo wake kwa ajili ya kutatua matatizo ya hapa na matatizo ya Kimataifa” aliongeza Mkapa.

Kwa upande wake Waziri Mkuu Mstaafu Jaji Joseph Sinde Warioba alisema kuwa sifa za uongozi bora ni pamoja kuthamini utu, uzalendo, uchapakazi na aliye na hofu ya Mungu.

“Sifa ya kiongozi bora ni lazima awe mtu anayethamini utu wa mtu na anayeamini binadamu wote ni sawa, awe mzalendo, muadilifu, mchapa kazi na ana hofu ya mungu,anashirikiana na kuwashirikisha viongozi wenzake." Alisema Jaji Warioba.
Naye Makamu Mwenyekiti  wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Bara, Phillip Mangula alisema kuwa cheo ni dhamana unayopewa na wananchi hivyo kiongozi bora ni yule atakaye ongoza kwa usawa.

”Cheo ni dhamana unayopewa na wananchi ili uweze kuongoza kwa usawa kwani kiongozi bora atawaongoza watu kwa usawa,” alisema Mangula.

Mangula alisema kuwa katika kipindi cha uongozi wa Mwalimu Nyerere alikuwa ni kiongozi anayejali sana wananchi wake akiamini kuwa binadamu wote ni sawa jambo ambalo analiona linajirudia katika Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Rais Dkt. John Pombe Magufuli ambaye naye amejipambanua kwa kuwajali wanyonge.


Kongamano hili lililohudhuriwa na viongozi mbalimbali wastaafu wakiongozwa na Rais Mstaafu Benjamin Mkapa, Salim Ahmed Salim,Spika Mstaafu Anne Makinda, Jaji Warioba, Jaji Agustino Ramadhan, na baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa nchini.Kauli mbiu ya Kongamano hilo ilikuwa ni “Urithi wa Mwalimu Nyerere Katika Uongozi, Maadili ya Uwajibikaji Kwenye Ujenzi wa Taifa.”

Post a Comment

0 Comments