Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack
akizungumza na wafanyakazi wakati wa kilele cha Siku ya Wafanyakazi kimkoa
ambayo ilifanyika katika uwanja wa Kambarage mkoani humo.
Sehemu ya watumishi wa Halmashauri ya
Wilaya ya Kishapu kutoka Chama cha Wafanyakazi wa Serikali la Mitaa (TALGWU) wakiwa katika maandamano kuingia uwanjani.
Mgeni rasmi, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,
Zainab Telack (wa pili kushoto) akifuatilia maandamano ya wafanyakazi wa sekta
mbalimbali walipokuwa wakipita mbele yake. Wengine pichani kuanzia kulia ni KatibuTawala
wa Mkoa wa Shinyanga, Albert Msovela, Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Nyabanga
Taraba, Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Fadhili Nkulu na Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga,
Josephine Matiro.
Gari la Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco)
Mkoa likiongoza magari ya taasisi zingine kupita mbele ya mgeni rasmi na
wafanyakazi kuonesha shughuli zinazofanya wakati wa sherehe za Mei Mosi.
Watumishi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa kutoka
Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya (TUGHE) wakiwa katika maandamano.
Mgeni rasmi, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,
Zainab Telack (wa tatu kulia) akiwa na Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Josephine
Matiro (wa pili kulia) wakiserebuka muziki aina ya kwaito pamoja na wafanyakazi kutoka sekta
mbalimbali.
Wafanyakazi kutoka halmashauri mbalimbali
mkoani Shinyanga wakishindana kuvuta kamba ikiwa ni mojawapo ya burudani wakati
wa sherehe hiyo.
Sehemu ya wafanyakazi wakifuatilia matukio
yaliyokuwa yakijiri uwanjani hapo.
MEI MOSI SHINYANGA
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack
amewataka wafanyakazi kutumia fursa zilizopo kwa kujituma katika uzalishaji ili
kupata malighafi zitakazotumika katika viwanda.
Telack alitoa rai hiyo juzi kwa wafanyakazi
mbalimbali mkoani hapa wakati wa kilele cha maadhimisho ya sikukuu ya Wafanyakazi
(Mei Mosi) kimkoa yaliyofanyika kwenye uwanja wa Kambarage.
Alisema wafanyakazi mbali ya kufanya kazi
za kuajiriwa pia wana nafasi ya kujiendeleza kwa kilimo cha mazao mbalimbali ili
viwanda vyetu vipate malighafi ya kutengenezea bidhaa.
Mkuu huyo wa mkoa alishauri kila mfanyakazi
akiweza angalau awe na ekari moja kwa ajili ya kilimo badala ya kutegemea tu
mshahara wa mwisho wa mwezi hali itakayochangia uchumi wa viwanda.
Aliwaagiza wakurugenzi na wakuu wa wilaya
waweke mkakati wa kuwapatia watumishi wao maeneo ili waweze kutumia fursa ya
kufanya kilimo kuwa sehemu ya kazi.
Mbali ya kuwapongeza wafanyakazi, kwa
upande mwingine, Telack aliwataka watumishi wajenge utamaduni wa kuheshimian
katika maeneo yao ya kazi na kuepuka migogoro isiyo na tija ili kuleta ufanisi
katika kazi.
Aliwaagiza waajiri wa sekta binafsi kutatua
kero za wafanyakazi wao ndani ya wiki mbili na kuhakikisha wanatekeleza maagizo
yanayotolewa na Serikali kuhusu sekta ya ajira.
Telack alibainisha kuwa akishirikiana na
Katibu Tawala wa Mkoa ataunda kamati sekta binafsi zote zenye changamoto kwa
wafanyakazi wao kuhakikisha kuwa zinazitatua mara moja.
Pia alivitaka vyama vya wafanyakazi viwe
sehemu ya kutetea wafanyakazi na si kugeuka kuwa wanaharakati hali inayoweza
kuchangia migogoro na waajiri wao.
Sherehe hizo zilizoambatana na maandamano
ya wafanyakazi wa sekta mbalimbali pamoja na burudani zilihudhuriwa pia na wakuu
wa wilaya za mkoa huo, wakurugenzi wa mamlaka za serikali za mitaa na viongozi
wengine mbalimbali.
Sherehe hizo kitaifa kwa mwaka huu
zilifanyika mkoani Kilimanjaro ambapo mgeni rasmi alikuwa Rais John Magufuli
zikiwa na kaulimbiu ‘Uchumi wa viwanda uzingatie haki, maslahi na hesma ya
wafanyakazi’.












0 Comments