Waziri wa TAMISEMI George Simbachawene ametangaza kujiuzulu nafasi yake
kutokana na kutajwa kwenye ripoti za uchunguzi wa tanzanite na almasi.
Akiwasilisha ripoti yake kwa Waziri Mkuu Bungeni Dodoma, Mwenyekiti wa
Kamati Maalumu ya Bunge iliyoundwa kuchunguza biashara ya madini ya
tanzanite, Dotto Biteko, alisema Simbachawene aulizwe ni kwa nini alitoa
uhamisho wa hisa za Sky Associate bila kuhusisha wataalamu kwa sababu
kamati ilishindwa kuelewa ni kwa nini alifanya hivyo.
“Kwa muktadha huo, ridhaa iliyotolewa Januari 30, mwaka 2015 na
aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini wa wakati huo, George
Simbachawene, ina dosari za kisheria na ukiukwaji wa kiutendaji na
utoaji wa ridhaa hii, unainyima Stamico kipaumbele cha kununua Kampuni
ya TML.
“Kwa msingi huo, kamati imebaini dosari zilizofanywa za kubadilisha
watoa maamuzi wa Kampuni ya TLM, zilifanyiwa kazi katika ngazi ya Wizara
ya Nishati na Madini chini ya Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Kamishna wa
Nishati na Madini na idara za sheria na katika mashauriano hayo,
yafuatayo yalibainika.
“Matokeo ya kuuza hisa Tanzanite One South Afrika, unaipa nguvu Kampuni
ya Sky Associate katika Kampuni ya TLM na mauziano hayo yasingeweza
kukamilika bila ya kupata kibali cha mheshimiwa waziri.
“Wizara ya Nishati na Madini ilitakiwa kabla ya kutoa ridhaa, ifanye
upembuzi yakinifu ili kujua mbia anayeondoka kama anadaiwa chochote
kabla ya kuruhusu uhamishaji wa wanahisa, lakini pia kuangalia uwezo wa
mbia anayekuja na kujiridhisha maamuzi ya wale wanaouza.
“Tarehe 30 Januari, waziri aliamua kutoa ridhaa bila ya kuzingatia
ushauri wa mwanasheria wa Wizara ya Nishati na Madini na katika hilo,
kuna barua ya ushauri wa mwanasheria iliyosema uuzwaji wa hisa hizo sio
halali kwa sababu mtu huyo hatumfahamu.
“Pili, Kamishna wa Madini alitoa ushauri kwa waziri, kwamba hili jambo
lisifanyike kwani utaratibu haujazingatiwa na pia Kamati ya Nishati na
Madini ikiwa chini ya Mheshimiwa Ndassa, ilitoa ushauri ikiwataka
wafuate utaratibu.
“Jambo linalosikitisha ni kwamba mheshimiwa Waziri Simbachawene
aliapishwa tarehe 24 na tarehe 27 akaingia ofisini na tarehe 30,
akasaini hati hiyo bila kuzingatia ushauri uliokuwapo.

0 Comments