Na Mwandishi Wetu-Dar es Salaam
Katika kuelekea maadhimisho ya wiki
ya wazazi CCM kitaifa chama hicho kimeandaa mkutano mkuu wa jumuiya ya wazazi
wilaya ya ilala ukilenga kuadhimisha miaka 62 tangu kuanzishwa Kwa
jumuiya hiyo.
Akizungumza katika mkutano huo
uliofanyika jijini Dar es salaam Mwenyekiti wa wazazi mkoa Frank Kamugisha
amesema kuwa lengo la kuanzishwa Kwa jumuiya hiyo ni kusimamia maadili, elimu,
afya, mazingira na mahusiano katika jamii.
Aidha ameupongeza uongozi wa wazazi
wilaya Kwa kuweza kuandaa mkutano huo,huku akibainisha kuwa atahakikisha katika
ngazi zote za chini kunafanyika mikutano na semina ili kuweza kutimiza azma ya
kuwa viongozi na kukiletea chama ushindi daima.
"Ajenda yetu kubwa ni tukae
katika taifa ambalo lina maadili mema kwa ajili ya ustawi wetu,kwani tunaweza
kufikia katika maendeleo ambayo Mwenyekiti wetu wa chama anakusudia kuyaona
katika jamii zetu",alisema Kamugisha.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa wazazi
wilaya ya Ilala Lucas lutainurwa amesema kuwa mkutano mkuu ni siku ya kuongea
juu taarifa ya kazi ambayo imeandaliwa kwa kipindi walichofanya kazi,huku
akieleza kuwa katika ziara iliyoandaliwa wilayani wamefanikiwa kutembelea
katika kata 36.
Lucas ameeleza kuwa lengo la ziara
hiyo ni kuwaeleza wajumbe juu ya umuhimu wa wiki ya wazazi, kuangalia uhai wa
jumuiya na kuhimiza suala zima la ulipaji wa ada kwa wanachama.
"Katika ziara yetu tumeweza kutembelea majimbo yetu yote matatu likiwa Jimbo la segerea,Ilala na ukonga,na nawahimiza viongozi kuweza kushuka katika mashina ili kuweza kujua matatizo yaliyopo",alisema.
Naye Katibu wa wazazi wilaya ya Ilala Sophia Abdul amesema kuwa baadhi ya matarajio ya jumuiya hiyo ni kuenzi juhudi zilizoanzishwa na Mwenyekiti wa wazazi taifa, kuunganisha makundi mbalimbali ya vijana katika malezi bora,kubuni miradi ili kuimarisha uchumi na kulinda mali za wazazi wilaya.
Amesema kuwa jumuiya hiyo inasimamia mambo yote ya kijamii hivyo itatatua changamoto wanayokumbana nayo wazee katika suala zima la bima za afya,utoaji wa ruzuku Kwa kaya masikini na miundombinu mibovu.
"Wazee wengi wamepata bima lakini wakienda hospitali wanapewa panadol hivyo tutafanyia kazi jambo hilo sambamba na kutoa ruzuku kwa kaya masikini kwa wale wanaostahiki",Sophia.
Hata hivyo amempongeza Rais John Pombe Magufuli na Mwenyekiti wa CCM Taifa kwa kazi kubwa ya kusimamia na kutekeleza ilani ya uchaguzi ya chama kwani Tanzania ya viwanda inawezekana.


0 Comments