Random Posts

Mkoa wa Tabora Kuwapa Chanjo ya Kinga ya Saratani ya Shingo ya Kizazi Wasichana 32,164

 Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri akisisitiza jambo wakati akifungua kongamano la siku moja la wadau wa afya lilokuwa likiwaelimisha juu ya maandalizi ya chanjo ya kuwakinga wasichana na saratani ya shingo ya kizazi jana mjini Tabora. Chanjo hiyo inazinduliwa tarehe 23 Mwezi huu.
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tabora Dkt . Gunini Kamba akitoa maelezo juu ya uendeshaji wa chanjo  ya kuwakinga wasichana dhidi ya  saratani ya shingo ya kizazi  wakati wa kongamano la wadau wa afya jana mjini Tabora. Chanjo hiyo inazinduliwa tarehe 23 Mwezi huu.

NA TIGANYA VINCENT
RS TABORA

ZAIDI  wasichana elfu 30 wenye umri wa miaka ( 14 ) wanatarajiwa kupata chanjo ya kinga ya Saratani ya mlango wa kizazi mkoani Tabora kuanzi wiki ijayo.
Kauli hiyo ilitolewa jana mjini hapa na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tabora(RMO) Gunin Patrick Kamba wakati wa kongamano la siku moja na wadau wa afya.
Alisema kuwa chanjo hiyo maalumu kwa watoto wa kike wenye umri wa miaka 14 itazinduliwa Aprili 23 mwaka huu katika Manispaa ya Tabora na Mkuu wa Mkoa kwa niaba ya maeneo mengine mkoani humo.
Dkt. Gunini alisema kuwa serikali imechukua hatua za makusudi kutoa chanjo hiyo ya saratani ya mlango wa kizazi kwa watoto wa kike kwani uchunguzi umebaini kwamba kundi hili ndilo lenye hatari ya kupata maambukizi kwa urahisi.
Mganga Mkuu huyo wa mkoa aliongeza kuwa lengo la Serikali ni kuwapatia chanjo watoto wa kike wa kuanzia miaka tisa lakini kwa kuanzia watakaohusika ni wenye miaka 14 ikiwa ni njia mojawapo ya kupunguza vifo vya akinamama vinavyosababishwa na saratani.
Aliongeza kuwa kinachochangia kuwepo kwa tatizo hilo kwa wingi ni pamoja na akina mama wengi kutofika kwenye vituo vya afya kupima.
Awali akifungua kongamano hilo Mkuu wa Mkoa huo Aggrey Mwanri alisema Serikali haitasita kuwachukulia hatua wale wote watakaokwamisha kwa namna moja ama nyingine utekelzaji wa zoezi hilo.
Mwanri alisema  kuna baadhi ya watu kwa makusudi ama kwa kutokujaa wanaopotosha wakidai kuwa chanjo hizi zinazotolewa kwa watoto kwamba ni kinga ya uzazi zitawafanya wasizae kumbe sio kweli na kuwaweka katika hatari.
Aidha aliwatadharisha watumishi wote wanaosimamia zoezi la mkubwa kwani haitasita kuchukua hatua kwa yeyote atakayejaribu kwa namna moja au nyingine  kukwamisha.
Alisema kuwa Chanjo hiyo inagharama kubwa wanaopotosha wanakusudia kuisababishia hasara Serikali na kuwaweka wasichana katika hatari na hivyo watachukuliwa hatua wakibainika.
Mkuu huyo wa Mkoa alitoa wito kwa wazazi kuwahimiza mabinti zao kujitokeza kwa wingi ili kupata chanjo hiyo kwa sababu kinga ni bora kulikoa tiba ili hatimaye wasalimike na madhara yatokanayo na Saratani ya shingo ya uzazi.

Chanjo hiyo ya kukinga saratani ya mlango wa kizazi (HPV Vaccine), ilizinduliwa hivi karibuni na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan kwenye viwanja vya Mbagala Zakhem jijini Dar es Salaam.

Post a Comment

0 Comments