Random Posts

Nyumba Karibia 80 Zawekwa x Kitongoji cha Janga

 Afisa ardhi halmashauri ya Kibaha ,Frenk Mwalembe akiweka X nyumba zilizo maeneo hatarishi nyakati za mvua  katika kitongoji cha Janga kata ya Janga ,ikiwa ni agizo la mkuu wa wilaya ya Kibaha ,Assumpter Mshama (Picha na Mwamvua Mwinyi)
 Moja ya nyumba zinazowekwa  X  maeneo hatarishi nyakati za mvua  katika kitongoji cha Janga kata ya Janga ,ikiwa ni agizo la mkuu wa wilaya ya Kibaha ,Assumpter Mshama ,katika zoezi hilo nyumba 50 zilizowekwa X na nyingine karibia 30 zipo ndani ya maji ambazo zitawekwa X .(Picha na Mwamvua Mwinyi)
Mkuu wa wilaya ya Kibaha ,Assumpter Mshama (wa kushoto) akizungumza kwenye zoezi la kuweka X nyumba zilizo maeneo hatarishi nyakati za mvua  katika kitongoji cha Janga kata ya Janga . (Picha na Mwamvua Mwinyi)

Na Mwamvua Mwinyi,Kibaha

SERIKALI wilayani Kibaha ,Mkoani Pwani imeweka X katika nyumba karibia 80 ,kitongoji cha Janga ,kata ya Janga ambazo zipo eneo hatarishi nyakati za mvua .

Aidha imetoa tahadhali na kuweka wazi kuwa hawatotoa kibali kwa wakazi hao ambao nyumba zao zipo kwenye hatari ya kusababisha madhara wakati wa mvua zinazoendelea kunyesha ama zijazo.

Akitoa rai hiyo ,wakati alipokwenda kwenye kusimamia zoezi la kuweka X kwenye nyumba hizo ,mkuu wa wilaya ya Kibaha ,Assumpter Mshama ,alisema zilizowekwa X ni 50 na nyingine zimeshindwa kufikiwa kutokana kuwa katikati ya maji ya mvua.

Alieleza , wananchi walioguswa wawe na amani na kuondoa hofu juu ya zoezi zililowapitia na badala yake wasubiri kusikia jibu la maamuzi ya serikali .

Hata hivyo ,Assumpter alisema kwasasa watatoa maeneo bure kuwahamisha wakazi hao ambapo watatakiwa kujenga wenyewe.

"Serikali haijawahi kuumiza wananchi wake ,kuweni na subira ,tunaangalia cha kufanya kwasasa na kusubiri majibu ya wataalamu wetu kuona itakavyokuwa"

"Wale ambao nyumba zao zipo kwenye maji kabisa msijidanganye mtapewa kibali kabisa ,kuhusu kuweka mtaro wa kutoa maji msikurupuke subirini wataalamu"

"Wataalamu tutawachukua wizarani na hao ndio watatujibu kama inawezekana kuweka mtaro huo ,msije kutia fedha halo,Msijichangishe kwasasa hadi wataalamu waseme majibu yao" alifafanua.

Assumpter alieleza endapo wataalamu watasema kunahitajika zaidi ya mil.200 ni vyema fedha hizo zitumike kwenye ujenzi mahala watakapohamishiwa .

Pamoja na hayo ,aliwataka kuondoka kwasasa kupisha mvua kwani amekuta mtu yupo kama ufukweni jambo ambalo ni hatari .

Pia mkuu huyo wa wilaya ya Kibaha ,alisema mtumishi yeyote atakaeenda kuwachangia chochote wasikubali labda kama mtumishi huyo atakuwa na barua itaonyesha imetoka ofisini kwao.

Nae afisa ardhi halmashauri ya Kibaha ,Frenk Mwalembe ,alisema amepokea agizo la kuweka X nyumba hizo kutoka kwa mkuu wa wilaya ili kujua idadi ya nyumba ambazo zipo eneo hatarishi .

Alisema miaka ya nyuma eneo hilo lilikuwa linachimbwa visima ,ni eneo ambalo maji hayana njia ya kutokea kwa wakati mmoja" na eneo hilo lipo nje ya utaratibu wa mipango miji, "alisema Mwalembe.

Mwalembe alisisitiza kwamba, ni vyema wakazi hao wakaondoka ili kuondokana na kero wanayoipata .

Mkazi ambae amekumbwa na adha hiyo ,luteni kanali mstaafu wa jeshi Angolile Mwakajinga ,aliomba serikali ikubali wachangishane kuweka mtaro mkubwa wa kudumu utakaopeleka maji mto Mkalamo .

Alisema gharama ni kubwa lakini ni vyema kuweka mtaro huo kuliko hasara ya kupewa viwanja bure ambapo watahitajika kwenda kujenga nyumba upya wakati wengine uwezo huo hawana.

Nyumba zaidi ya 30 zimezungukwa hadi sasa bila kuwa na njia ya kutoka maji ambayo yametokana na mvua zilizonyesha wiki hii, kitongoji cha Janga.

Post a Comment

0 Comments