Random Posts

Vifo Vinavyotokana na Malaria Vyapungua Mkoani Pwani

 Mkuu wa mkoa wa Pwani, mhandisi Evarist Ndikilo akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kampeni ya uhamasishaji wa kununua na kutumia dawa zinazozalishwa katika kiwanda cha Tanzania Biotech Product Ltd kilichopo Kibaha, itakayofanyika april 12 mwaka huu ,huko Mailmoja.
 Mganga mkuu wa mkoa wa Pwani, Yudas Ndungile (wa kwanza kulia) akizungumza na waandishi wa habari katika kikao kilichokiitisha mkuu wa mkoa wa Pwani, mhandisi Evarist Ndikilo (wa kushoto)kuelezea kampeni ya uhamasishaji wa kununua na kutumia dawa zinazozalishwa katika kiwanda cha Tanzania Biotech Product Ltd kilichopo Kibaha, itakayofanyika april 12 mwaka huu ,huko Mailmoja

Baadhi ya waandishi wa habari mkoani Pwani wakimsikiliza kwa makini mkuu wa mkoa huo,mhandisi Evarist Ndikilo ,ofisini kwake wakati alipokuwa akielezea kampeni ya uhamasishaji wa kununua na kutumia dawa zinazozalishwa katika kiwanda cha Tanzania Biotech Product Ltd kilichopo Kibaha, itakayofanyika april 12 mwaka huu ,huko Mailmoja
Picha na Mwamvua Mwinyi
……………………
Na Mwamvua Mwinyi,Pwani
VIFO vinavyotokana na ugonjwa wa malaria katika mkoani Pwani, vimepungua kutoka 124 kwa mwaka 2016 na kufikia  vifo 57 sawa na asilimia 9.6 mwaka 2017.

Pamoja na hilo ,kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka 2015 -2017 wagonjwa wa malaria walioripotiwa katika zahanati ,vituo vya afya na hospitali mkoani humo ,walikuwa 720,181.

Hayo yalibainika katika kikao cha mkuu wa mkoa wa Pwani, mhandisi Evarist Ndikilo ,kilichomkutanisha na waandishi wa habari ,kuelezea kampeni ya uhamasishaji wa kununua na kutumia dawa zinazozalishwa katika kiwanda cha Tanzania Biotech Product Ltd kilichopo Kibaha, itakayofanyika april 12 mwaka huu ,huko Mailmoja .

Alieleza  ,kutokana na takwimu hizo ugonjwa huo bado  ni  hatari hivyo wamejipanga kuhamasisha na kuongeza matumizi ya dawa ya viuadudu ili kudhibiti mbu waenezao malaria.

“Kwa kuzingatia kwamba kiwanda cha dawa hizi kipo hapa kwetu na kuwa maambukizi ya malaria kimkoa bado yapo juu takriban asilimia 15 zaidi ya maambukizi ya kitaifa ambayo ni asilimia 14,  tumedhamiria kuongeza matumizi ya dawa hiyo” 

“Kwa uzoefu kwa wenzetu nchini Cuba ambao walianza kutumia viuadudu vya kuua mbu wa malaria kabla yetu wamefanikiwa kutokomeza kabisa gonjwa hilo ” alisema Ndikilo.

Ndikilo alisema ,katika uhamasishaji huo wanakusudia kufanya mambo mawili ikiwemo kuujuliaha umma kuwa dawa ya kutokomeza malaria ipo Kibaha kwa kutoa elimu kwa vitendo ya matumizi na kuzigawa dawa hizo bure kwa baadhi ya wananchi.
Alifafanua dawa hizo zitakazogawiwa bure zimenunuliwa na Jumuiya ya wafanyabiashara Mkoani Pwani kwa gharama ya milioni 1.056 ili wananchi hao waondokane na malaria .

“Lengo la kampeni hii ni muendelezo wa utekelezaji wa agizo la Rais dkt.John Magufuli alilolitoa wakati wa ziara yake kiwanda hicho June 22 mwaka jana ,ambapo aliagiza kila halmashauri Tanzania Bara kununua dawa hii  na kuipulizia kwenye maeneo yenye mazalia ya mbu “alifafanua.

Hata hivyo ,Ndikilo aliagiza wakurugenzi wa halmashauri zote na wananchi kujitokeza kukunua dawa ili kupambana na mbu kwenye maeneo yao.

Nae mganga mkuu wa mkoa wa Pwani, Yudas Ndungile ,alisema licha ya takwimu kuonyesha ugonjwa wa malaria kushuka kimkoa lakini jamii iendelee kujikinga na kutumia njia nyingine kama dawa ,vyandarua  ili kukabiliana na ugonjwa huo.

Alielezea ugonjwa unaoongoza kwa sasa kimkoa ni magonjwa yanayotokana na mfumo wa hewa ,ikifuatiwa na malaria.

Ndungile alisema ,mwaka 2016 ugonjwa wa malaria ulikuwa ukiongoza lakini kwasasa umeshuka na kuwa wa pili hivyo kuonyesha idadi ya vifo navyo kupungua.

Post a Comment

0 Comments