Taasisi
ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kipindi cha miezi mitatu ya Januari hadi
Machi 2018 imeona jumla ya wagonjwa 19,371 wenye matatizo mbalimbali ya moyo
kati ya hao wagonjwa wa nje ni 18,481 na waliolazwa ni 890.
Wagonjwa
105 walifanyiwa upasuaji wa moyo wa kufungua kifua kati ya hao watu wazima 53 na watoto 52. Kati ya wagonjwa
105 waliofanyiwa upasuaji 66 walifanyiwa na madaktari wetu bingwa wa
magonjwa ya moyo watoto wakiwa ni 35 na
watu wazima 31.
Upasuaji wa moyo wa bila kufungua kifua
(Catheterization) kwa kutumia mtambo wa Cathlab ulifanyika kwa wagonjwa 231 kati ya hao watoto ni 20 na wakubwa 211. Kati
ya wagonjwa 231 waliotibiwa wagonjwa
watu wazima 211 walifanyiwa upasuaji na madaktari wetu wa ndani.
Kwa
kipindi cha miezi mitatu tumekuwa na
jumla ya kambi za matibabu nane (8) ambapo
tulifanya matibabu kwa kushirikiana na washirika wetu kutoka nchi za Ujerumani,
Israel, Australia , Marekani, India na Falme za Kiarabu. Katika kambi hizo jumla
ya wagonjwa 39 walifanyiwa upasuaji wa kufungua kifua kati ya hao watoto 17 na
watu wazima 22. Wagonjwa 72 walifanyiwa
upasuaji wa bila kufungua kifua kati ya hao watoto 20 na watu wazima 52.
Tumefanya upasuaji wa kuunganisha mishipa ya damu (AVF-
Arterio Venous Fistula) kwa ajili ya kusafishia damu kwa wagonjwa wenye
matatizo ya figo (Hemodialysis) 36.
Changamoto
kubwa tunayokabiliana nayo ni wagonjwa wengi tunaowapokea mioyo yao kutokuwa
katika hali nzuri hivyo basi tunawaomba wananchi kujenga tabia ya kupima afya zao mara kwa mara
hii itawasaidia kujuwa kama wana matatizo ya moyo au la na kama
wanamatatizo wataweza kupata tiba kwa
wakati.
Wazazi
na walezi tunawaomba wasisahau kupima afya za watoto wao pale watakapoona kuna
hali ya tofauti katika ukuaji wa mtoto kwani magonjwa mengi ya moyo yanaanzia
utotoni. Mtoto akianza kuuguwa magonjwa ya moyo wazazi wengi wanadhani ni
matatizo ya kifua baada ya kumfikisha Hospitali na kufanyiwa vipimo ndipo inagundulika mtoto anasumbuliwa na magonjwa
ya moyo. Kwa wamama wajawazito wafanye uchunguzi (Fetal Echocardiography) wa
kuangalia kama mtoto aliyeko tumboni anamatatizo ya moyo.
Aidha
kwa upande wa gharama za matibabu Taasisi yetu imeyagawa katika makundi manne (4) tuna wagonjwa
wanaotibiwa kwa bima mbalimbali ambazo tumeingia makataba nazo. Wagonjwa
wanaolipia gharama zote wenyewe, wagonjwa wanaochangia kidogo huku gharama zingine zikilipwa na Serikali.
Kundi la mwisho ni wagonjwa ambao
hawalipii kabisa gharama za matibabu ikiwa watakidhi vigezo vyote vya kutokulipa.
Huduma
zetu za matibabu ya moyo zinatolewa kwa
watanzania wote wa Bara na Visiwani. Ifahamike kwamba fedha za matibabu zinazolipwa na wagonjwa
zinatumika kununua vifaa tiba vya moyo kama mlango wa moyo (Valve), betri ya moyo (Pacemaker) na vinginevyo.
Kutokana
na matibabu ya moyo kuwa ya gharama kubwa tunaendelea kuwasisitiza wananchi
wajiunge na mifuko ya bima za afya ambayo itawasaidia kulipa gharama za
matibabu pindi watakapohitaji kutibiwa. Pia itasaidia Hospitali yetu kuendelea
kujiendesha yenyewe kwa kushirikiana na Serikali na wadau wengine.
Imetolewa
na:
Kitengo
cha Uhusiano
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
19/04/2018

0 Comments