Random Posts

Wanawake Waungane Kukimbilia Fursa-Lwanji

 Afisa maendeleo ya jamii katika halmashauri ya Mji wa Kibaha ,Leah Lwanji (wa kushoto )akipokea zawadi kutoka kwa kikundi cha Pwani Generation Queens ,wakati wa sherehe yao ya mwaka mmoja ya kikundi,wa tatu kutoka kulia ni mwenyekiti wa kikundi hicho Betty Msimbe.(Picha na Mwamvua Mwinyi)
 Mwenyekiti wa kikundi cha Pwani Generation Queens, Betty Msimbe (wa kulia)akizungumza wakati wa sherehe ya kikundi hicho kufikisha mwaka mmoja. 
Baadhi ya wanachama wa kikundi cha Pwani Generation Queens wakifungua shampen wakati wa sherehe ya kusheherekea mwaka mmoja wa kikundi hicho. (Picha na Mwamvua Mwinyi)

Na Mwamvua Mwinyi,Pwani

AFISA maendeleo ya jamii katika halmashauri ya Mji wa Kibaha ,Leah Lwanji amewataka wanawake kuacha kulalamika kukosa fursa ya mikopo ngazi ya halmashauri na badala yake wajiunge kwenye vikundi ili kuwezeshwa kirahisi.

Aidha ametoa rai kwa wale wanawake wajasiriamali waliopiga hatua kiuchumi na wenye uwezo kuthubutu kuwekeza kwa kuanzisha viwanda vidogo vidogo na hata vikubwa .

Leah alitoa rai hiyo wakati wa sherehe za kufikisha mwaka mmoja wa kikundi cha Pwani Generation Queens-  Kibaha mkoani Pwani, ambacho kina wanachama 75 hadi sasa.

Alieleza wakati umefika kwa wanawake wajasiriamali kukimbilia fursa,kujikubali ,kujiamini na kuthubutu ili kujiinua kimaendeleo na kuacha utegemezi ndani ya familia.

Leah alisema ,wapo baadhi ya akinamama wajasiriamali wadogo ambao bado hawajanufaika na fungu la asilimia 10 ya mapato ya ndani ambalo hukopeshwa wanawake,vijana,wazee na walemavu.

"Hakuna mtu ama mjasiriamali mmoja mmoja atakaepewa fedha hiyo mkononi bila utaratibu wowote "

"Nawaomba tusilalamike na kutupia lawama halmashauri,serikali,taasisi binafsi pekee ,kwani utaratibu wa kupata fedha hizi unajulikana ,ni lazima muungane vikundi ,muache ubinafsi ili hali mpate fursa hii kirahisi" alisisitiza Leah.

Afisa maendeleo huyo ,alielezea idara hiyo kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo wameweza kutoa mafunzo ya ujasiriamali kwa wajasiriamali 751 ambapo kati yao wanawake ni 480 .#

Hata hivyo Leah alisema, mwaka 2016-2017 halmashauri ilitoa fedha kiasi cha sh.mil .173 kwa ajili ya mikopo kwa wanawake na vijana  ,2017-2018 ilitoa mil.368 na July -Sept 2017 walitoa mil.100 kwa vikundi 50 vyenye wanachama 320.

Aliupongeza muungano huo ,na kuwaomba wazidi kuwa wamoja ,waache majungu na fitna kwa lengo la kusonga mbele,kuinua umoja wao.

Mwenyekiti wa Pwani Generation Queens ,Betty Msimbe alisema wapo kikatiba ,wana akaunti na fedha ya akiba sh. mil .Tisa huku wakiendelea na miradi midogo .

Alisema wanachama wake ni kuanzia miaka 18 na kuendelea wakiwa ni wakazi wa maeneo ya wilaya ya Kibaha,Kisarawe na Ubungo .

Betty alisema, lengo la kikundi ni kushirikiana katika mipango ya kimaendeleo, shida na raha na kuwezeshana. 

Mwanachama wa kikundi hicho ,Zarina Zenzele alisema endapo watashirikiana wanaamini nia na malengo ya kikundi yatafikiwa. 

Aliomba serikali na taasisi mbalimbali za kijamii kuwaunga mkono ili waweze kuwezeshwa na kupiga hatua kiuchumi.

Post a Comment

0 Comments