Subscribe Us

header ads

Balozi Dr. Augustine Mahiga Akutana na kufanya Mazungumzo na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi

 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dr. Augustine Mahiga akisalimiana na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alipofika nyumbani kwake Bara bara ya Haile Selassie Jijini Dar es salaam kubadilishana mawazo.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif akisisitiza jambo wakati wa mazungumzo yake na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dr. Augustine Maiga akiwa kwenye Makaazi yake Bara bara ya Haile Selassie Jijini Dar es salaam.
.......................................................

Waziri ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dr. Augustine Mahiga amesema Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itasimamia ipasavyo na kuhakikisha kwamba nia ya Mahujaji wa Tanzania waliojiandikisha kwenda kutekeleza Ibara ya Hijja Nchini Saudi Arabia Mwaka huu inatimia.

Amesema Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki inafuatilia hatua za mwisho katika kuona tatizo lililojitokeza kwa baadhi ya Taasisi za Usafirishaji Mahujaji upande wa Tanzania Bara kukabiliwa na madeni Nchini Saudi Arabia linapata ufumbuzi wa haraka kabla ya kumalizika kwa muda wa mwisho wa uthibitisho wa Mahujaji wa Mwaka huu.

Balozi Dr. Augustine Mahiga amesema hayo wakati alipofika katika Makazi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Bara bara ya Haile Selassie Jijini Dar es salaam kubadilishana mawazo kuhusu masuala ya Hijja yaliyoleta usumbufu mwaka jana kwa Mahujaji wa Tanzania.

Amesema atalazimika kuzungumza na Mufti  Mkuu wa Tanzania pamoja na Uongozi wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) ili kujua hatua walizofikia katika kuona Taasisi zinazosimamia usafirishaji Mahujaji upande wa Bara wamemaliza matatizo yanayowakabili.

Balozi Mahiga alimthibitishia Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba uongozi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki utalazimika kutoa baraka kwa Mahujaji wanaosimamiwa na Taasisi za Zanzibar kwanza wakati zile za Tanzania Bara  zitashugulikiwa baadaye baada ya kumaliza changamoto zao.

Hatua ya Balozi Mahiga imekuja kufuatia baadhi ya Taasisi za Usafirishaji Mahujaji za Tanzania Bara kushindwa kulipa Madeni na kupelekea Wizara inayosimamia masuala ya Hijja Nchini Saudi Arabia kutishia kuzuia Mahujaji wa Tanzania kuingia Nchini humo kwa Ibada ya Hijja Mwaka huu.

Akigusia Miradi ya Kiuchumi inayolenga kustawisha maendeleo ya Tanzania Waziri wa Mambo ya Nje na Afrika Mashariki Balozi Mahiga alisema ipo haja ya kufuatilia Miradi iliyopata Mikopo na ufadhili wa Kimataifa ili kujua maendeleo yake.

Balozi Mahiga aliitaja baadhi ya Miradi hiyo ni  pamoja na ile ya  Ujenzi wa Bandari ya Maruhubi kwa Mpiga Duri Kisiwani Unguja na ile ya Bandari  ya Wete Kisiwani  Pemba ambayo imo ndani ya Mpango Mkuu wa Miradi ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Naye kwa upande wake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alimpongeza Balozi Maiga kwa hatua alizoamua kuzichukuwa za kukabiliana na changamoto zilizojitokeza kwenye masuala ya Hijja.

Balozi Seif alisema Ibada ya Hijja ni miongoni mwa Nguzo Tano wanazowajibika Waumini wa Dini ya Kiislamu wenye uwezo kuzitekeleza ambayo imo ndani ya Imani za Waumini jambo ambalo wasimamizi wa masuala hayo wanalazimika kuwa makini katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Akielezea furaha yake kutokana na uamuzi wa Tanzania kuweka nia ya kutaka kufungua Ubalozi wake Nchini Jamuhuri ya Cuba, Balozi Seif  alisema hatua hiyo muhimu itaongeza chachu ya uhusiano wa Kihistoria uliopo kati ya Tanzania na Cuba.

Balozi Seif alisema Cuba ni Taifa la kwanza lililoyatambua na kuyaunga mkono Mapinduzi ya Zanzibar ya Mwaka 1964 na imekuwa ni mshirika mkubwa kwa Tanzania hasa katika kusaidia Taaluma kwenye miradi iliyomo ndani ya Sekta zaKilimo, Afya na hata masuala ya Viwanda.


Habari na picha kwa hisani ya Ofisi ya Makamu
wa Pili wa Rais wa Zanzibar na
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki-Ofisi ya Zazibar

26/06/2018

Post a Comment

0 Comments