Subscribe Us

header ads

Vikundi 13 Kupewa Mkopo Unaotokana na Fedha za Mapato Ya Ndani

..................................
Na Mwandishi Wetu.

Vikundi 13 vikiwemo vya akina mama, vijana na Watu wenye ulemavu vilivyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi vimepewa mafunzo ya kuwajengea uwezo juu ya usimamizi wa miradi ikiwa ni hatua ya kuviandaa kwaajili ya kupewa mikopo isiyo na riba inayotokana na asilimia 10 ya makusanyo ya fedha za mapato ya ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya jamii Wilaya ya Bariadi Bi. Beatrice Gwamagobe amebainisha kuwa katika awamu hii vikundi vipatavyo 13 vinatarajia kupatiwa mikopo isiyo na riba ambapo jumla ya Shilingi Milioni 130 zitatolewa kama mkopo kwa vikundi hivyo.

Aidha alitoa mchanganuo kuwa Shilingi Milioni 74 zimetokana na asilimia kumi ya makusanyo ya mapato ya ndani kwa robo ya kwanza 2022/2023, Milioni 44 zimetokana na marejesho ya vikundi vilivyokopeshwa awamu zilizopita na Shilingi  Milioni 12 ni bakaa kutoka Mwaka wa fedha 2021/2022 hivyo jumla kufanya kiasi cha Shilingi milioni 130.

“Leo tulikuwa na mafunzo kwa vikundi kumi na tatu ambavyo vinakwenda kupewa mikopo, vikundi kumi ni vya wanawake, viwili vya vijana na kimoja cha watu wenye ulemavu, vikundi hivi vinajishughulisha na shughuli mbalimbali za ujasiriamali kama vile Kilimo, Ufugaji, Biashara na shughuli nyinginezo zinazoingiza kipato” alifafanua Bi. Beatrice

Naye Bi. Sophia Charles mmoja miongoni mwa wanakikundi kiitacho “Wanawake wapiganaji” kutoka kijiji cha Mbugani kata ya Banemhi amebainisha kuwa mafunzo waliyopewa yamewasaidia kuwaongezea uelewa juu ya namna ya kuendesha miradi yao ili iweze kuwapa faida ambayo pia itawasaidia kufanya marejesho ya mkopo wao kwa wakati.

Sambamba na vikundi hivyo kupewa mafunzo Afisa Sheria wa Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi Bw. Raymond Cosmas aliviongoza vikundi hivyo katika utiaji wa saini wa mikataba ya mikopo hiyo na kuhakikisha vipengele vyote vimeeleweka na vimeridhiwa.

Post a Comment

0 Comments