Thursday 26 October 2023

Dk. Mahenge : utulivu, amani, Siasa Safi umeongeza uwekezaji nchini

Mkurugenzi wa kiwanda cha  Wild Flower,Grains and Oil Mill Project, Khalid Omary akimuonesha Mwenyekiti wa Bodi ya Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) Dk. Binilith Mahenge (wa pili kulia) mfumo wa maji wakati alipotembelea kiwanda hicho Oktoba 26, 2023. Wa tatu kutoka kulia ni Mjumbe wa Bodi TIC, Mhandisi Peter Chisawillo.
Ukaguzi wa kiwanda hicho ukiendelea.
Mafundi wa kiendelea na kazi ya ujenzi wa kiwanda hicho.
Ukaguzi wa kiwanda hicho ukiendelea.
Mwenyekiti wa Bodi ya Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) Dk. Binilith Mahenge, akizungumza na Mkurugenzi wa Kiwanda  cha Kuchambulia Pamba cha Biosustain (T) Limited , Sajiad Haider.
Muonekano wa wa Kiwanda cha kusindika mafuta ya alizeti cha Maunt Meru Millers.
Muonekano kwa nje wa Kiwanda cha kusindika mafuta ya alizeti cha Maunt Meru Millers.
Mkurugenzi wa Kiwanda cha kusindika  mafuta ya Alizeti cha Mount Meru Miller's  Sree Valsan Nair (katikati) akitoa maelekezo kwa Mwenyekiti wa TIC wakati wa ukaguzi wa kiwanda hicho.
Kikao na viongozi wa kiwanda cha usindikaji mafuta cha Maunt Meru Millers kikiendelea.
Mkurugenzi wa  Kiwanda cha Kuchambulia Pamba cha Biosustain (T) Limited kilichopo mjini Singida, Sajiad Haider akisisitiza jambo wakati wa ukaguzi wa kiwanda hicho.
Lori likipakia pamba katika kiwanda hicho.
Muonekano wa baadhi ya mashine za kuchambua pamba katika kiwanda hicho.
............................

 Na Dotto Mwaibale, Singida

UTULIVU amani na siasa safi chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan umeongeza uwekezaji hapa nchini kutoka wawekezaji 20 waliokuwa wakisajiliwa kwa mwezi hadi kufikia 80.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) Dk. Binilith Mahenge wakati  akizungumza baada ya kutembelea kiwanda cha kusindika mafuta cha Wild Flower,Grains and Oil Mill Project kilichopo nje kidogo ya Manispaa ya Singida wakati wa ziara yake ya kuhamasisha uwekezaji wa ndani aliyoifanya Oktoba 26,2023.

" Utulivu, amani na siasa safi inayofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan imekuwa kivutio kikubwa cha wawekezaji kuja nchini kuwekeza na ni jambo la kujivunia," alisema Dk.Mahenge.

Alisema kutokana na hali hiyo idadi ya wawekezaji wanaosajiliwa TIC inaendelea kuongezeka kila siku baada kuanza kutekelezwa kwa sheria mpya ya uwekezaji ya mwaka 2022 ambayo imepunguza thamani ya mtaji unaohitajika kwa mwekezaji wa ndani kutoka Dola za Kimarekani 100,000 hadi 50,000 kwa ajili ya kuwavutia wawekezaji wa ndani.

Alisema sheria hiyo namba 10 ya 2022 inatambua wawekezaji mahiri nakupewa vivutio vya uwekezaji na kuwa wale wenye sifa wanapewa misamaha ya kodi kwa  kuwa ndani ya kipengele hicho cha umahiri.

Alisema hivi sasa suala zima la uwekezaji limebadilika kwa kasi kubwa na Rais Samia Suluhu Hassan kuonekana ni namba moja kutokana na nchi kuwa na sheria hiyo ambayo inawavutia wawakezaji wengi.

Dk. Mahenge alitumia nafasi hiyo kuwahamasisha  watanzania wenye mitaji mikubwa kwenda TIC kujisajili ili waweze kutambulika jambo litakalo ongeza idadi ya wawekezaji hapa nchini.

Mkurugenzi wa kiwanda cha  Wild Flower,Grains and Oil Mill Project, Khalid Omary, alisema kiwanda hicho kitakapo kamilika ujenzi wake kitatoa ajira za kudumu na za muda mfupi kwa wananchi kati ya 400 hadi 1,000 na kuwa uwekezaji wake ni zaidi ya Sh.bilioni 56.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kiwanda cha kusindika  mafuta ya Alizeti cha Mount Meru Miller's  Sree Valsan Nair alisema baada ya kutambuliwa kuwa muwekezaji mahiri mwaka 2013 alipata msamaha wa kodi kwa kuondolewa VAT kwa mafuta anayouza lakini aliendelea kulipa kodi na sasa anaomba alipwe Sh.Bilioni 12 ambazo alikuwa akizilipa licha ya kutambuliwa kuwa ni mwekezaji mahiri.

Nair alisema wamefungua kiwanda cha kutengeneza sabuni kutokana na mabaki ya malighafi zingine zinazopatikana baada ya kukamuliwa kwa mbegu za alizeti na kuongeza ajira kwa wananchi hatua ambayo imepongezwa na Mwenyekiti wa TIC Dk. Mahenge.

Mkurugenzi wa  Kiwanda cha Kuchambulia Pamba cha Biosustain (T) Limited kilichopo mjini Singida, Sajiad Haider alisema changamoto kubwa walionayo ni umeme ambao unakatwa kwa zaidi ya saa nane na Shirika la  Umeme Tanzania (TANESCO) jambo ambalo limepunguza uzalishaji.

Changamoto ya pili aliyoitoa ni kuhusu eneo lao lenye mgogoro ambapo ameomba vyombo vinavyoshughulikia suala hilo kulimaliza ili waweze kuliendeleza na kupata sehemu ya kuhifadhi pamba yao.

Mwenyekiti wa Bodi ya TIC Dk. Binilith Mahenge katika ziara hiyo aliongoza na mjumbe wa bodi hiyo Mhandisi Peter Chisawillo, Meneja wa TIC Kanda ya Kati Venance Mashiba, Kaimu Katibu Tawala Msaidizi sehemu ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida, Lucas Mkuki na Afisa Uwekezaji Masungu Mdanya kutoka TIC Kanda ya Kati.

Viwanda vilivyotembelewa na Dk.Mahenge ni kiwanda cha kusindika mafuta cha Wild Flower,Grains and Oil Mill Project,  Kiwanda cha Kuchambulia Pamba cha Biosustain (T) Limited na Kiwanda cha kusindika mafuta ya Alizeti cha Mount Meru Miller's  ambapo kesho atahitimisha ziara yake kwa kuzungumza na Serikali ya Mkoa wa Singida, kutembelea mgodi wa Dhahabu wa Shanta uliopo Wilaya ya Ikungi na kukutana na wawekezaji waliopo mkoani hapa.

No comments:

Post a Comment