Habari za Hivi Punde

6/recent/ticker-posts

Header Ads Widget

SHIRIKA LA SPRF LAJIVUNIA MAFANIKIO YA MIAKA 10, RC SINGIDA ALIPONGEZA

Muonekano wa keki ya  maadhimisho ya miaka 10 tangu lianzishwe Shirika lisilo la Kiserikali la Stars of Poverty Rescue Foundation (SPRF) lenye makao makuu yake Mkoa wa Singida.
Mgeni rasmi Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida, Yagi kiaratu, akiwa  amefuatana na Mwenyekiti wa bodi ya Wakurugenzi ya SPRF, Redempter Rweyemamu (kulia) wakiwasili katika ukumbi wa Social mkoani Singida wakati wa  maadhimisho ya miaka 10 ya  Shirika lisilo la Kiserikali la Stars of Poverty Rescue Foundation (SPRF).
Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida, Yagi kiaratu akizungumza wakati wa  maadhimisho ya miaka 10 tangu lianzishwe Shirika lisilo la Kiserikali la Stars of Poverty Rescue Foundation (SPRF). Kiaratu alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Singida, Halima Dendego.
--------------------------------------------------------------------
Dotto Mwaibale,na Solomon Philemon. Singida

SHIRIKA lisilo la Kiserikali la Stars of Poverty Rescue Foundation (SPRF) lenye makao makuu yake Mkoa wa Singida linajivunia mafanikio ya miaka 10 tangu kuanzishwa kwake huku likijipambanua kwa kuendelea kuwa na mipango kabambe kuanzia mwaka huu wa 2025 hadi ifikapo 2030.

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida, Yagi kiaratu akizungumza Disemba 31, 2024 kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Singida, Halima Dendego ambaye alikuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya miaka 10 tangu shirika hilo lianzishwe aliwapongeza watendaji wa SPRFkwa kutimiza miaka hiyo chini ya maono ya kuwa kitovu cha ubora katika kutokomeza umaskini kwa Afya na ustawi.

“Mimi sikuifahamu vizuri SPRF, lakini nimeelezwa, nimejifunza, nimeelewa  na ninafahamu kwamba, SPRF imejielekeza katika kutokomeza umaskini kwa njia mbalimbali kama kutoa elimu za stadi za maisha, ujuzi na biashara kwa makundi ya kijamii, kutoa huduma za afya, ikiwemo huduma za afya ya uzazi na magonjwa ya wanawake, uhamasishaji wa matumizi ya maji safi na salama na utunzaji wa mazingira,” alisema Kiaratu.

Kiaratu alitaja kazi nyingine zinazofanywa na shirika hilo kuwa ni kuanzisha vituo vya afya na programu za elimu ya afya katika kusaidia watu na vikundi vilivyo katika mazingira hatarishi, kutekeleza kanuni za utawala bora kwa kupinga ukatili wa kijinsia kwa vitendo, kuweka misingi ya ukuzaji wa ujuzi na ubunifu kwa wafanyakazi wake, washirika na wanufaika inaowahudumia na kufanya mafunzo, ufuatiliaji, tathmini ya program zake na utafiti kwa takwimu zao za mafanikio.

Kiaratu alisema kupitia mawasilisho mbalimbali amejifunza jinsi SPRF inavyoweza kuchangia katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2025.

“ Wote tunatambua kwamba madhumuni ya Dira ya Taifa ya maendeleo ya 2025 ni kufikia maisha ya hali ya juu kwa watu wake kupitia utawala bora utawala wa sheria na kuendeleza uchumi imara na shindani na kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan anaitekeleza azima hiyo kwa vitendo,” alisema Kiaratu kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa.

Aidha, Kiaratu alisema pamoja na SPRF kutekeleza MKUKUTA katika kuisaidia Serikali kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2025, pia inatekeleza malengo matatu makuu ya maendeleo Endelevu ya Dunia kwa vitendo.

Aliyataja malengo hayo kuwa ni lengo la kwanza la Dunia la Maendeleo Endelevu (SDGs) linalosema NO POVERTY (yaani kusiwepo umaskini) akitolea mfano SPRF inavyotafuta fedha kujenga mradi wa soko eneo la Kideka katika Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi, kusadia wanawake 100 kiuchumi katika kupunguza umaskini wa kaya. Pia Mkurugenzi wake anakusudia kujenga ofisi za asasi ya SPRF Mkoa wa Singida.

Alitaja lengo la tatu la Dunia la Maendeleo Endelevu linahusu AFYA na Ustawi wa jamii [yaani Good Health & well Being] ambapo SPRF inatoa huduma za afya kwa wananchi wa Singida. Kwa mwaka 2025 inakusudia kupanua wigo wa huduma kwa kuanzisha kliniki ya uzazi  na chanjo (PRIDE RCH) hapa mjini Singida, ambapo pia wameombwa na Manispaa kusaidia kazi hiyo.

Alitaja lengo la tano la Dunia la Maendeleo Endelevu ni kuleta usawa wa Kijinsia [Gender equality] kwa kupinga ukatili dhidi wanawake na watoto zikiwemo  aina zingine zote za ukatili; ambapo tumeona, SPRF inatekeleza Mpango wa Taifa wa kutokomeza ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto (MTAKUWWA) katika hali na sura zote kwa vitendo ikishirikiana na washirika wengine.

“ Kuna mashirika mengi yanayopinga ukatili na ninaamini kwamba nguvu ya pamoja ni muhimu zaidi mkishirikiana katika kutekeleza kazi hii muhimu kwa jamii,” alisema.

Kiaratu alisifia mpangilio wa kazi na ustadi wa mawasiliano kwenye ngazi za Mkoa, Halmashauri na Mamlaka ya Serikali za Mitaa na vijiji vikihusika katika kumwezesha mwananchi kupinga ukatili na kuleta maendeleo kupitia mradi wa AWARE uliotekelezwa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi.

“ Naipongeza SPRF kwa kuendelea kuwepo Singida na kutekeleza miradi ya kijamii kwa miaka 10 iliyopita. Siyo kazi rahisi kufanya kazi za kujamii bila kuwa na msaada wa kifedha.

Nawapongeza tena SPRF kwa kutembelea wagonjwa hospitali ya Manispaa  na kutoa misaada kwa wahitaji na hasa akina mama waliojifungua wakiwemo; Kama vile haitoshi mlitembelea pia wafungwa na mahabusu katika Gereaza la Singida mjini na kutoa misaada ya kiutu katika kufanya maadhimisho ya kutimiza miaka 10 tangu kuanzishwa kwa shirika lenu la SPRF,” alisema Kiaratu.

Kiaratu katika hafla hiyo alizindua kitabu cha Usimamizi wa Biashara na Ujasiriamali kilichoandikwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika hilo, Dr.Suleiman Charles Muttani na kueleza kuwa anaamini kitabu hicho  kitakuwa chachu ya mafunzo kwa mradi wa Wanawake 100 ambao umeasisiwa na SPRF kwa nia njema ya kuwatoa wanawake juani na kuwaweka kivulini kwa kujenga soko eneo la  Kideka kwa msaada wa wananchi na wadau wengine.

Katika hatua nyingine Kiaratu aliendesha harambee ya uchangishaji fedha kwa miradi ya Kideka wenye thamani ya Sh.8,733,750/=) na mradi wa Wanawake 100 wenye thamani ya Sh. 6,560,200.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa bodi ya Wakurugenzi ya SPRF, Bi. Redempter Rweyemamu alisema lengo kuu la taasisi hiyo ni kusaidia Serikali katika kutekeleza MKUKUTA na DIRA ya Taifa ya Maendeleoya 2025  yakiwemo maendeleo endelevu ya Dunia SDGs ifikapo 2030 mikakati ambayo haijaeleweka sana ngazi za jamii.

Rweyemamu alitaja malengo makuu ya Asasi ya SPRF ni  Kutengeneza mazingira wezeshi katika kuchukua hatua za punguza umaskini wa kipato  hasakwa kuimarisha uchumi wa kaya,  kuweka mifumo yenye kusaidia watu, makundi athirika na jamii katika kuondokana na umaskini kwa kuanzisha programu za elimu na afya ili kusaidia mtu mmoja mmoja na makundi yaliyo katika mazingira hatarishi na magumu.

Alitaja lengo lingine kwa upande wa afya kuwa, SPRF inatoa huduma za Afya kwa magonjwa ya wanawake, afya ya uzazi, mama na mtoto; sambamba na hayo SPRF inahamasisha usawa wa kijinsia, haki za Wanawake na watoto.  SPRF pia inahamasisha ushirika na taasisi za kitaifa na kimataifa kwenye juhudi za pamoja katika kuchukua hatuaendelevu za kuondoa umaskini nchini Tanzania na kwingineko.

Akielezea dhana ya shirika hilo; alisema ni kuwezesha, kukuza na kuhifadhi utu, haki za binadamuna utawala bora ili kuondoa umaskini na kuleta maendeleo ya kaya na kwamba kama nchi hatutaweza kuzungumza uchumi wa nchi bila kuimarisha uchumi wa kaya ama kuacha mila na desturi zilizopitwa na wakati zikitamalaki.

Mwenyekiti huyo wa bodi ya wakurugenzi akizungumzia mradi wa AWARE alisema  halijawahi kuwa jambo rahisi kwa watu wenye mitazamo na mapokeo tofauti kuacha mila zao na kuwafanya watu hao wenyewe wapinge mila zao wenyewe ambazo kwa kiasi Fulani zinazorotesha maendeleo.

“Tulishuhudia SPRF ikiwashirikisha watu mahala pamoja na kuwafanya kuzungumza lugha yao na hatimaye wenyewe kuwa kipaza sauti dhidi ya mila potofu ya Ukeketaji ndoa na mimba za umri mdogo, ukatiliwa kijinsia kwa wanawake na watoto. Kazi ambayo ni kati ya sababu ya kukutana leo tukiadhimisha miaka kumi,” alisema Rweyemamu.

Rweyemamu akizungumzia miaka 10 ya shirika hilo alisema imejengwa katika kujitoa kwa nia thabiti kuitumikia Jamii, kwa moyo na kwa nguvu zao zote na kuwa anatambua hamu kubwa ya wadau katika kusaidia kutokomeza umaskini wa kipato na kuwa na jamii inayotambua kazi kama kipimo cha utu.

Halikadharika alisema anatambua kwamba Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2025 inaisha na tutaanza Dira ya Taifa ya 2050 na baada ya kuwa tutaendelea na malengo ya dunia ifikapo (SDGs) 2030.

Alisema anaiona SPRF kama mfano halisi wa asasi za kiraia; ikilenga kuendeleza juhudi halisi katika kwenda na Dira mpya ya maendeleo ya nchi ya 2050 na agenda ya Afrika 2063 ambapo asasi zote zinapashwa kwenda kwenye uelekeo huo kwa ajili ya kujenga asasi imara na watu makini.

Naye Mkurugenzi wa SPRF Dr. Suleiman Muttani akizungumzia kazi za  shirika hilo alisema ni kutoa elimu ya stadi za maisha, ukuzaji ujuzi na ubunifu katika kupunguza  umaskini  na linatoa huduma za elimu ya afya kwa jamii.

Alitaja kazi nyingine ni kuhamasisha usawa wa kijinsia na kupinga ukatili wa aina zote, kujenga uwezo wa kitaasisi kwa kushirikiana na wadau wake kokote duniani na kuiwezesha jamii kutokomeza  umaskini kwa na ustawi kwa wote.

Dr. Muttani aliongeza kuwa SPRF kama mojawapo ya Asasi za Kiraia (AZAKI) ni taasisi kamili yenye jukumu la kufanya kitu fulani katika kuimarisha ama kuboresha maisha ya watu mahali iliko.   Kwamba kuwa kazi kuu ya azaki yoyote duniani ni kulinda ubinadamu na ustawi wa watu Mahali lilipo kwa kujielekeza kwenye kusudio Maalum ya kazi zake.

Aidha, Dr. Muttani alisema matarajio ya shirika hilo kwa mwaka 2025-2030 ni kuendelea  kuchukua hatua za kupunguza umaskini wa kaya, kuendeleza  program za elimu na afya katika kusaidia makundi athirika kwenye Jamii, kuendeleza  ushirikiano na wanajamii, taasisi za kitaifa na kimataifa katika kutafuta fedha za kujenga miundombinu za ujasiria mali Singida,kuendelea  na kujenga uwezo wa kitaasisi katika kukua na kuwa azaki endelevu.

Alitaja kazi zinazotarajiwa kufanywa na shirika hilo kuwa ni kufundisha ujasiriamali  kwa wanawake 100 wanaojitambua ifikapo Disemba 2027, kujenga  soko dogo kwa ajili wa wanawake wanaofanya biashara eneo la Kideka ili kuwapunguzia kuungua na jua katika hatua za kupunguza umaskini wa kaya kwa uchangishaji wa fedha kutoka jumuia za ndani kwa ajili ya kupata fedha za ujenzi wa mradi huo wenye thamani ya Sh. 8,733,750 watatumia  fomu maalum kwa ajili ya kuzipata hadi ifikapo  ifikapo  Disemba 2027 ama kabla.

Alitaja kazi nyingine kuwa watapanua wigo wa huduma za afya kwa kuanzisha kliniki kwa wajawazito na  chanjo  katika ofisi za sasa za PRIDE polyclinic ili kuwahudumia wajawazito na watoto kwa ufanisi zaidi kuanzia mwezi Machi, 2025.

Kazi nyingine wanayotarajia kuifanya ni kuanzisha ujenzi wa ofisi ya shirika hilo mkoani Singida kabla ya Disemba 2030, kutafuta fedha kwa ajili ya mradi wa AWARE hatua ya II kutoka kwa wadau wengine ili kutekeleza dhana ya utawala bora na kupinga ukatili wa aina zote, kuhamasisha uwepo wa usalama wa chakula kwa kuzingatia utunzaji wa mazingira na kupunguza athari zitokanavyo na Mabadiliko ya tabia nchi.

Alitaja baadhi ya changamoto ni ukosefu wa fedha za kuendeshea miradi ya kijamii, kwa kuishiwa mbinu ama uwezo wa utafutaji fedha kama utegemezi kutoka mataifa ya kigeni, ukosefu wa watumishi walio tayari kutekeleza kazi za jamii kwa malengo tuliojikwekea, mawasiliano dhafifu na jamii hasa jamii kutokujua kazi zinazofanywa na asasi za kiraia kama SPRF.

Dr. Muttani alitumia nafasi hiyo kueleza kuwa SPRF itaendelea  kujitanabaisha na Jamii wanayoihudumia kama nyenzo ya kufahamika na iwe tayari  kuchangia miradi ya kijamii.

Mkurugenzi wa SPRF Dr. Suleiman Muttani akizungumzia kazi zinazofanywa na   shirika hilo. Mwenyekiti wa bodi ya Wakurugenzi SPRF, Redempter Rweyemamu akielezea malengo makuu ya taasisis hiyo.Mratibu wa Mradi wa Shirika hilo, Mwadinuu Kassim akifafanua kuhusu miradi iliyotekelezwa na shirika hilo.Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida, Yagi Kiaratu akikata utepe kuzindua kitabu cha "USIMAMIZI WA BIASHARA NA UJASIRIAMALI" kilichoandaliwa na Mkurugenzi wa SPRF Dr. Suleiman Muttani.Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida, Yagi Kiaratu akionesha kitabu hicho mara baada ya kukizindua (kulia) ni Mkurugenzi wa SPRF Dr. Suleiman Muttani.Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida, Yagi Kiaratu (kulia) akimkabidhi kitabu Mkurugenzi wa SPRF Dr. Suleiman Muttani.Mkurugenzi wa SPRF Dr. Suleiman Muttani akizungumza mara baada ya kukabidhiwa kitabu hicho.  Mwenyekiti wa bodi ya Wakurugenzi SPRF, Redempter Rweyemamu (kushoto) Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida, Yagi Kiaratu (katikati) Mkurugenzi wa SPRF Dr. Suleiman Muttani wote kwapamoja wakikata keki iliyoandaliwa kwa ajili ya maadhimisho ya miaka 10 tangu lianzishwe Shirika lisilo la Kiserikali la Stars of Poverty Rescue Foundation (SPRF)Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida, Yagi Kiaratu akimlisha keki Mkurugenzi wa SPRF Dr. Suleiman Muttani.Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida, Yagi Kiaratu akimlisha keki Mkurugenzi wa Kampuni ya MIU Food Products, Dr. Micky Ulaya.Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida, Yagi Kiaratu, Mkurugenzi wa Kampuni ya  MIU Food Products,Dr. Micky Ulaya wakimkabidhi tunzo ya kuwajengea uwezo kibiashara Mkurugenzi wa SPRF Dr. Suleiman Muttani .Mkurugenzi wa Kampuni ya  MIU Food Products, Dr. Micky Ulaya, na Mkurugenzi wa SPRF Dr. Suleiman Muttani wakiwa kwenye picha ya pamoja na tuzo hiyo maalumu.Wageni waalikwa wakiwa kwenye maadhimisho hayo.Mwenyekiti wa CCM Wilaya Singida Mjini, Lucia Mwiru (kulia) akisalimiana na Mkurugenzi wa SPRF Dr. Suleiman Muttani (katikati) Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida, Yagi Kiaratu.Wageni waalikwa wakiwa kwenye maadhimisho hayo.Picha ya pamoja baada ya maadhimisho hayo.Taswira ya Muonekano wa Soko  KIDEKA 

Post a Comment

0 Comments