Na Benedict Liwenga, MAELEZO-Dodoma.
MUUNGANO
wa Tanzania ni muungano wa damu na wa watu, ambapo Ibara ya kwanza Sura
ya kwanza inaeleza kuwa msingi mkuu wa Jamhuri ya Muungano pamoja na
katiba iliyopo na inayopendekezwa ni haki ya makubaliaono ya mwaka 1964.
Hayo
yamesemwa leo na Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Mary Nagu
wakati akichangia mada katika mjadala ndani ya bunge hilo kuhusu mambo
mchakato mzima wa kusaka Katiba Mpya.
Mhe.
Nagu amesema kuwa Hati ya Makubaliano hayo imejengeka katika misingi ya
utu, udugu na kuaminiana ambapo Waasisi wa muungano huo hawakupeleka
maslahi yao wenyewe binafsi wala kuzingatia suala la mali, bali
walizingatia umuhimu na mahitaji ya muungano kutokana na mambo hayo
makuu matatu.
Ameeleza kuwa mambo wanayoyajadili bungeni hapo kwa sasa ndiyo yatatokana na muungano ambao una mfumo bora na muundo bora.
Mhe. Nagu amebainisha kuwa wale viongozi wenye kutaka muungano wenye gharama kubwa watawafanya wengine washindwe hapo baadaye.
“Naomba
sana tuendelee na kuona kuwa muungano huu ni muhimu nataka niwaambie
kwamba Zanzibar ni lango kuu la Jamhuri ya muungano wa Tanzania na lango
hili linatuhakikishia usalama wetu na ulinzi wetu kwahivyo na
Wazanzibar nao wanufaike na rasilimali za Bara, kwahiyo muungano huu ni
muhimu na utanufaisha pande zote mbili mimi sina wasi wasi”, alisema
Mhe. Nagu.
Aidha, Mhe. Nagu amegusia suala la usawa wa jinsia kupitia hamsini kwa hamsini katika uwakilishi, ajira na maeneo mengine.
Mhe.
Nagu ameleza kuwa usawa wa jinsia utajenga jamii nzuri ya Tanzania
ikiwemo kuleta heshima pamoja na haki katika jamii hiyo kwani kwa mila
na desturi za Waafrika na Watanzania, wanaume hawakupaswa kuwa wamiliki
wa kila kitu.
“Akina
baba ni Custodians lakini wakajigeuza wamiliki, tunachotaka waendelee
kuwa Custodians na sisi watuone ni wenzao, kwahivyo suala la jinsia
halina mjadala, kupitia uwakilishi teundelee na hamsini kwa hamsini na
Katiba iseme wazi, mengine yatajitokeza kwenye Sheria ya uchaguzi”.
Alisisitiza Mhe. Nagu.
Kuhusiana
na suala la ajira na uongozi Mhe. Nagu ameeleza kuwa wanawake zaidi ya
asilimia 52% wangepaswa kuwa katika kila eneo lakini hawapo na suala
hilo linaleta tofauti isipokuwa mashambani ambapo chakula chote
kinachotoka kwa kiasi kikubwa wanaolima ni wanawake.