Random Posts

WADAU WATAKA SOMO LA SANAA LIRUDISHWE SHULENI

3.... (1) 
Kaimu Katibu Mtendaji wa Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) Godfrey Mngereza akijumuika na Kikundi cha Sanaa cha watoto cha Blessed Hill kutoa burudani kwenye Jukwaa la Sanaa la Baraza hilo lililofanyika mapema wiki hii. 4 
Msanii mkongwe wa Sanaa za Maonesho Bakari Mpelemba maarufu kama Mzee Jangala (Kulia) akifuatilia kwa makini burudani za ngoma za asili na maigizo zilizokuwa zikitolewa na kikundi hicho cha Blessed Hill sambamba na wadau wengine wa Sanaa.
2. (1) 
Kikundi hicho kikiendelea kuonesha manjonjo ya ngoma mbalimbali za asili kwenye Jukwaa la Sanaa
Na Mwandishi Wetu
Wadau wa Sanaa wameeleza kusikitishwa na kudumaa kwa utamaduni na mwamko mdogo miongoni mwa watanzania katika kuthamini utamaduni huku wakitoa wito kwa Serikali kufikiria kurejesha masomo ya Sanaa katika mitaala ya shule za msingi kama ilivyokuwa zamani.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti kwenye Jukwaa la Sanaa la Baraza la Sanaa la Taifa lililofanyika mapema wiki hii kwenye viwanja vya Baraza hilo, wadau hao walisema kwamba ni muda muafaka sasa wa kujenga misingi ya Utamaduni kutoka ngazi za chini hasa mashuleni ili kuepuka kutokomea kwa utamaduni wa mtanzania.
“Tunahitaji kujiuliza kama tunataka kupata utambuzi wa mtanzania au kukubali kupoteza utamaduni wetu. Hakuna jinsi kama taifa tunaweza kupiga hatua kama hatuthamini utamaduni na kuhakikisha watoto wetu na vizazi vijavyo vinarithi utamaduni wetu” alisisitiza msanii maarufu wa Sanaa za Maonesho Bakari Mpelemba maarufu kama Mzee Jangala.
Aliongeza kwamba, ni wajibu wa kila mmoja aliyepo sasa kuhakikisha anauona utamaduni kama urithi mkuu kwa watoto na vizazi vijavyo na kusisitiza kwamba kama jamii itashindwa kutimiza hili basi si ajabu vizazi vijavyo kuja kupiga viboko makaburi ya baba na mama zao.
Msanii mwingine mkongwe wa Sanaa za Maonesho Nkwama Bhallanga alisema kwamba muda umefika sasa kuanza kusukuma utambuzi wa mtaala wa Sanaa katika shule za msingi kwani ndiyo njia pekee ya kujenga jamii inayojitambua lakini pia uwezo wa kumudu masomo miongoni mwa watoto mashuleni.
“Sanaa huleta ukakamavu, huwajenga watoto katika misingi ya kujielewa na kuzingatia masomo yao mashuleni. Watoto wanaojikita kwenye sanaa na masomo mengine ni wepesi kufanya vizuri darasani pia” alisisitiza Ballanga.
Awali wakitoa burudani kwenye Jukwaa hilo, watoto wa shule ya awali na msingi ya Blessed Hill inayopatikana eneo la Kitunda, wilaya ya Ilala katika mkoa wa Dar es Salaam, waliigiza maigizo mbalimbali yaliyobeba maudhui ya kutoa wito kwa wadau wa Utamaduni kuanza kuthamini utamaduni na kuurithisha kwa watoto.

Post a Comment

0 Comments