Na Mwandishi wetu
................................................................
Muswada wa Sheria
ya Huduma za Habari wa mwaka 2016 umezingatia vigezo muhimu anavyopaswa kuwa
navyo mwanahabari ikiwemo weledi na maadili katika kutekeleza majukumu yake.
Hayo
yamesemwa leo na mwanataaluma mkongwe katika tasnia ya habari nchini Bw. Clement
Mshana wakati akitoa tathmini yake kuhusu muswada huo.
Bw. Mshana
ameeleza kuwa kutokana na mabadiliko makubwa ya sayansi na teknolojia hakuna
budi kuwa na sheria mpya kwenye tasnia ya habari ili kuendana na mabadiliko
hayo bila ya kuathiri maadili na miiko ya tasnia hiyo.
Alisema kuwa
makosa mengi ya kihabari yanayojitokeza hufanywa kwa makusudi ili kupotosha
jamii kama vile kuandika habari za uongo, hali hii inatokana na watu wasio na
sifa kuvamia fani kwa hiyo ni muhimu kuwe na vigezo maalum vya kumtambua
mwanahabari.
“Vyombo vya
habari vya leo sio vile vya miaka ya nyuma, kuna mabadiliko mengi na wanahabari
pia wamekuwa wengi wakiwemo baadhi ambao hawana sifa hivyo ni lazima kuwe na
mabadiliko ya sheria na muswada huu umezingatia vigezo vyote vya msingi ili
kuleta hadhi na heshima ya taaluma hiyo” alisema Mshana.
Pia Mshana
aliongeza kuwa muswada huo una vipengele vya muhimu katika kuboresha maslahi ya
wanahabari kama vile fursa za mafunzo, bima na hifadhi ya jamii mambo ambayo
yana faida kwao ukizingatia kwamba kazi yao ni nyeti na ina misukosuko mingi.
“Vipengele
vya bima na hifadhi ya jamii ni muhimu sana kwani vinalinda maslahi ya
wafanyakazi katika tasnia ya habari kwa sababu mara nyingine kazi hii ina
hatari lakini wamiliki wengi wa vyombo vya habari wanapenda kufanyiwa kazi bila
ya kujali maslahi ya wafanyakazi wao ndio maana wanapinga sheria hii kwa vile
itawabana” alifafanua Mshana.
Aidha,
Mshana amewataka baadhi ya wadau wa sekta ya habari kuacha kupotosha kwa kuwa muswada
huo ni mzuri na wadau walishirikishwa hivyo walipaswa kutoa maoni ya kuboresha badala
ya kupinga huku wakitetea maslahi ya watu wachache.
0 Comments