Waziri
Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali imetoa sh. bilioni 1.4 kati ya sh.
bilioni 1.8 zilizotengwa katika mwaka huu wa fedha kwa ajili ya uendelezwaji wa
mradi wa ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe.
Amesema
ujenzi wa hospitali hiyo ni utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM)
ya mwaka 2015/2020 ya kuwa na zahanati katika kila kijiji, kituo cha afya
katika kila kata, hospitali katika wilaya na hospitali za rufaa kwa kila mkoa.
Waziri
Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Jumamosi, Januari 21, 2017) wakati alipotembelea
eneo la mtaa wa Wikichi inapojengwa hospitali hiyo akiwa katika siku ya tatu ya
ziara yake ya kikazi mkoani Njombe.
Amesema
lengo la ujenzi wa hospitali hiyo ni kuhakikisha mwananchi anaanza kupata
huduma za afya katika eneo lake na anapokuwa na tatizo kubwa ndipo atakwenda
hospitali ya wilaya na kisha hospitali ya rufaa ya mkoa.
“Hospitali
hii ikikamilika itawapunguzia wananchi gharama za kusafiri umbali mrefu kwa
ajili ya kufuata huduma za rufaa. Sasa hakutakuwa na sababu ya kwenda Iringa,
Mbeya wala Ruvuma huduma zote zitakuwa zinapatikana hapa hapa Njombe,” amesema.
Amesema
ujenzi huo utakapokamilika Serikali itapeleka fedha za ununuzi wa dawa na vifaa
tiba. “Hatuwezi kukosa fedha za kununulia vifaa tiba na dawa kwani ni moja ya
majukumu yetu,”.
“Mheshimiwa
Rais Dkt. John Magufuli ameahidi kuwahudumia na kuwatumikia wananchi wote bila
ya kujali uwezo wao, itikadi zao za kidini na kisiasa na hapa ndiyo maana ya
ahadi hiyo ya Serikali ya kuwahudumia. Watu wote watakuja kutibiwa hapa,”
amesema.
Akitoa
taarifa ya ujenzi mradi wa hospitali hiyo, Katibu Tawala wa Mkoa wa Njombe, Bw
Jackson Saitabau amesema kukamilika kwa ujenzi wa hospitali hiyo kutawapunguzia
wananchi gharama kubwa za kufuata huduma za rufaa katika mikoa ya jirani.
Amesema
ujenzi wa hospitali hiyo ulianza katika eneo hilo lenye ukubwa wa takribani
ekari 70 katika mwaka wa fedha wa 2013/2014, ambapo kiasi cha sh. 953.705
zilitengwa kati yake sh. milioni 236.575 zilitumika kwa ajili ya ulipaji wa fidia.
“Hospitali
hii inajengwa kwa awamu na tulianza na jengo la wagonjwa wa nje (OPD) ambapo gharama
za mradi ni sh. bilioni 3.2 huku gharama za mtaalamu mshauri ni sh. milioni 114.160.
Mradi ulianza Julai 23, 2016 na unatarajiwa kukamilika Januari 26, 2018,”
amesema.
Amesema
kuwa hadi sasa kazi ya ujenzi huo imekamilika kwa asilimia 40 na mkandarasi
ameshalipwa sh. milioni 892.963 sawa na asilimia 28 ya gharama za mradi na
mtaalam mshauri amelipwa sh. milioni 51.50.
Naye
Mbunge wa Jimbo la Njombe, Mheshimiwa Edward Mwalongo ameishukuru Serikali kwa
kuwawezesha kupata hospitali ya Rufaa ya mkoa huo na amewaomba wananchi
waendelee kuiunga mkono Serikali na washiriki kikamilifu katika kuilinda
miundombinu hiyo.
Pia
Waziri Mkuu amezindua Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Wanging’ombe
iliyojengwa katika Kata ya Igwachanya pamoja na kupokea taarifa ya ujenzi wa
Ofisi hiyo pamoja na kuweka jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa Ofisi ya Mkuu
wa Wilaya ya Wanging’ombe.
Aidha,
Waziri Mkuu amewataka watumishi wa halmashauri hiyo ambao wananshi nje ya eneo
wilaya hiyo wawe wamehamia ifikapo Februari 15 mwaka huu.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
IJUMAA, JANUARI 20, 2017.
0 Comments