Naibu Katibu Mkuu wa
CCM Zanzibar Vuai Ali Vuai akiwahutubia
wanachama wa CCM katika Hafla ya Uwekaji wa jiwe la msingi Tawi la CCM Fuoni
Michenzani.
Baadhi ya Wana CCM wakila kiapo cha utii mara
baada ya kukabidhiwa kadi za kujiunga na Chama pamoja na Jumuiya Zake katika
hafla hiyo.
Naibu Katibu Mkuu wa
CCM Zanzibar Vuai Ali Vuai akizindua
jiwe la msingi katika tawi hilo la Fuoni Michenzani.
Vijana wa Chipukizi wakimvisha sikafu ya
heshima Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Vuai Ali Vuai mara baada ya kuwasili katika hafla hiyo.
Vijana wa sarakasi
wakionyesha uwezo wao mbele ya Naibu Katibu Mkuu wa CCM Vuai Ali Vuai katika
Hafla hiyo.
NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar kimewashauri wanachama wenye nia ya kugombea nafasi za
uongozi ndani ya chama na jumuiya zake kuhakikisha
wanakemea vikali na kuunga mkono kampeni za kuthibiti
dawa za kulevya nchini ili kuwanusuru
vijana wanaoathirika na janga
hilo.
Ushauri huo umetolewa na Naibu
Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Nd.Vuai Ali
Vuai katika hafla ya kuweka jiwe la
msingi kwenye Tawi la CCM Fuoni Michenzani
Unguja, alisema dawa za kulevya ni sawa na bomu la maangamizi linaloteketeza maelfu ya vijana na kupoteza nguvu kazi nchini.
Vuai alieleza kuwa ni lazima kila
mwanachama anayejiandaa kugombea nafasi ya uongozi ndani ya Chama hicho awe
tayari kukemea na kupinga hadharani matumizi ya dawa za kulevya nchini kwa
lengo la kuunga mkono juhudi zinazofanywa na viongozi wakuu wa Kitaifa akiwemo
Mwenyekiti wa Chama hicho Dkt. John Pombe Magufuli na Makamo Mwenyekiti wake
Dkt. Ali Mohamed Shein waliosimama imara kupambana vita hiyo.
Naibu Katibu Mkuu huyo alisisitiza
kwamba kukemea matumizi ya dawa hizo kwa viongozi wa serikali na Chama sio maamuzi
binafsi bali wanatekeleza ibara ya 155 ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM mwaka
2015/2020 inayoeleza kwa kina mikakati ya kupambana na kuthibiti dawa hizo
nchini kwa maendeleo ya wananchi wote.
Pia alisema ibara hiyo imeeleza
hatua ya kuundwa kwa Tume ya kuthibiti dawa za kulevya pamoja na kuanzishwa kwa
vituo vya matibabu ya kuwatibu watu
waliothirika na matumizi ya dawa hizo ikiwa ni hatua za kuwasaidia ambapo
serikali zote mbili zimetekeleza matakwa hayo kwa kuruhusu taasisi binafsi
kuanzisha vituo vya kurekebishia tabia (Soba house).
“Wanachama wenye nia ya kugombea
nafasi za uongozi ndani ya Chama na Jumuiya zetu lazima waonyeshe nia kwa
vitendo ya kupambana na dawa za kulevya
na tukimuona mtu ana kigugumizi na muhali wa kukemea vitendo hivyo basi atakuwa
hafai kuwa kiongozi kwani sote kwa sasa ni lazima tucheze wimbo mmoja katika
mapambano haya”,. Alisisitiza Vuai na kuongeza kuwa Dawa za kulevya ni Adui wa maendeleo ya nchi.
Hata hivyo aliwataka wanachama
hao kutumia vikao halali kama vyenzo ya kujadili masuala ya shughuli za chama
na kutafuta usuluhishi wa baadhi ya changamoto zinazojitokeza katika ngazi
mbali mbali za chama hicho na kuepuka tabia za kujadili mambo ya chama nje ya
vikao halali kwani kufanya hivyo kunatengeneza majungu na fitina.
Akizungumzia uchaguzi wa Chama
unaotarajiwa kufanyika hivi karibuni alisema kila mwanachama ana haki ya
kuchagua na kuchaguliwa hivyo watendaji watakaopewa majukumu ya kusimamia
mchakato huo watekeleze majukumu yao kwa mujibu wa Katiba ili kila mwanachama
mwenye nia apate haki yake kisheria.
“ Tunaingia katika uchaguzi wetu
ndani ya Chama na Jumuiya kwa wale wenye nia ya kugombea Mjue kuwa katika
mchakato wowote wa kisiasa hasa uchaguzi kuna kupata na kukosa hivyo tusije
kugawanyika kwa kuwa pengine umekosa au amepata usiyempenda.”, aliwasihi Vuai wanachama hao.
Sambamba na hayo aliwapongeza
viongozi na wanachama wa Tawi hilo kwa kutekeleza kwa vitendo matakwa ya
kikatiba ya Mradi wa Awamu ya Tatu unaoagiza Chama na jumuiya kutekeleza kwa
vitendo dhana ya Siasa na Uchumi kwa kujenga majengo ya kisasa yanayotoa fursa
za kufanyika miradi ya kiuchumi inayowanufaisha wanachama wote.
Pamoja
na hayo alitoa kadi kwa wanachama wapya waliojiunga na Chama na Jumuiya
zake na kuwataka wafuate maelekezo na taratibu na miongozo ya kikatiba
ndani ya chama hicho kwa lengo la kuleta ufanisi katika utelezaji wa
shughuli za chama.
Akisoma risala mwanachama wa Tawi
hilo Bi.Salhiya Ahmada alisema Tawi hilo limejengwa kwa msaada wa nguvu za wanachama
kwa kushirikiana na baadhi ya wahisani ndani ya chama hicho ambao ni makada wa
CCM akiwemo Makamo Mwenyekiti wa Chama hicho ambaye pia ni Rais wa Zanzibar
Dkt. Ali Mohamed Shein.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa
Jimbo la Fuoni Kichama ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Dimani Juma Ali Juma
alisema toka aingie madarakani amekuwa akitekeleza ilani ya CCM kwa kasi ambapo
mpaka sasa tayari ametekeleza kwa kiasi kikubwa ahadi alizowaahidi wananchi
ndani ya jimbo hilo.
Akizungumza Kada mkongwe wa CCM
ambaye pia ni Mshauri wa Raisi wa Zanzibar katika masuala ya Utamaduni na
Utalii Bw. Chimbeni Kheir Chimbeni
ambaye ni msimamizi mkuu wa Ujenzi wa Tawi hilio alitoa shukrani zake
kwa wadau mbali mbali waliotoa michango yao kufanikisha ujenzi wa tawi hilo
toka kununuliwa kwa kiwanja mpaka kusimamisha jengo hilo.
Katika hafla hiyo viongozi na wanachama
mbali mbali walichangia fedha na taslim na wengine kutoa ahadi ya fedha zaidi
ya milioni Tatu ambapo naibu katibu Mkuu
Vuai Ali Vuai kwa niaba ya Afisi Kuu Zanzibar aliahidi kuchangia shilingi
milioni mbili na kugharamikia baadhi ya
matengenezo ya miundombinu ya jengo hilo.





0 Comments