Random Posts

SIKU YA WANAWAKE DUNIANI, WAZIRI KAIRUKI AONGOZA KUFANYA USAFI MUHIMBILI

 Waziri Kairuki (wa pili kutoka kushoto) akifanya usafi katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) leo ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha siku ya wanawake duniani. Kushoto ni Mkurugenzi wa Uuguzi wa Muhimbili, Agness Mtawa. Kutoka kulia wa kwanza ni Katibu wa Umoja wa Wanawake katika Wilaya ya Ilala, Joyce Ibrahimu Mkaugala na Zuhura Mawona wakifanya usafi Leo katika hospitali hiyo.
 Waziri Kairuki akizungumza na kinamama waliojifungua watoto kabla ya kuwapatia zawadi ya nguo za watoto, pampazi na sabuni.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejementi ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mheshimiwa Angellah Kairuki akizungumza na wafanyakazi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) leo kabla ya kukabidhi vitanda 10 na magodoro 10 kwa uongozi wa hospitali hiyo. Katika kusherekea siku ya wanawake duniani leo, pia Waziri huyo amewapatia kinamama zawadi mbalimbali zikiwamo nguo za watoto na sabuni. Kushuto Mkurugenzi wa Uunguzi katika hospitali hiyo, Agness Mtawa.
 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejementi ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mheshimiwa Angellah Kairuki akikabidhi  vitanda 10 na magodoro 10 kwa Mkurugenzi wa Uuguzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Agness Mtawa.
 Mkurugenzi wa Uuguzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Agness Mtawa akimshukuru Waziri Kairuki baada ya kupokea msaada wa vitanda na magodoro leo.

Hospitali ya Taifa Muhimbili –MNH- leo imeungana na wanawake wengine ulimwenguni kote kuadhimisha siku ya wanawake Duniani kwa kufanya usafi katika maeneo mbalimbali ya hospitali hiyo.

Zoezi hilo limeongozwa na Mbunge wa Vitimaalum mkoa wa Dar es salaam Mheshimiwa Angellah Kairuki kwa niaba ya Umoja wa Wanawake wa Chama cha Mapinduzi –UWT- mkoani humo.

Mheshimiwa Kairuki ambaye pia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora amesema katika kusheherekea siku ya wanawake Duniani UWT  imeona ni vema wakashiriki katika shughuli mbalimbali za kijamii ili kuonesha dhamira ya dhati kwamba CCM inawajali wananchi wake bila kujali itikadi ya chama.

‘’ Sisi tumekuja hapa Muhimbili kushiriki na nyinyi katika kuadhimisha siku hii kwa kufanya usafi bila kujali itikadi ya chama kwani Hospitali hii inahudumiwa wananchi wote , pia  siku hii ya leo tunatoa msaada wa vifaa mbalimbali vya watoto na  wenzetu wengine wameenda katika Hospitali zingine wote tukiwa na lengo moja’’. Amesema Waziri Kairuki.

‘’Msaada tuliotoa ni  vitanda kumi, magodoro kumi , mashuka  na vifaa vingine mbalimbali vya watoto zikiwamo nguo ,sabuni na Pampers  lengo ni kuunga mkono juhudu za serikali za kuboresha huduma za afya hususani  afya ya mama na mtoto na kuhakikisha hakuna mgonjwa anayelala chini kwa kukosa kitanda’’ . Amesema Mheshimiwa Kairuki.

Akipokea msaada wa vitanda hivyo Mkurugenzi wa Huduma za Uuguzi na Ukunga wa MNH  Agnes  Mtawa amewashukuru UWT kwa msaada walioutoa ambao amesema umekuja wakati muafaka kwani utasaidia katika kutekeleza majukumu yao .

Hata hivyo Mkurugenzi Mtawa amewakumbusha wauguzi kuendelea kufanya kazi kwa kufuata maadili na kusisitiza kuwa kazi hiyo inahitaji kujitoa na kuwa na moyo wa huruma .

Siku ya wanawake Duniani huadhimishwa kila Machi nane ambapo kauli mbiu ya mwaka huu ni ‘’ Tanzania ya Viwanda , Wanawake ndio msingi wa mabadiliko ya kiuchumi .

Post a Comment

0 Comments