Jovina Bujulu-
MAELEZO.
............................................
Wanawake nchini
wametakiwa kujiwezesha kiuchumi, kijamii na kisiasa ili wapate fursa ya
kushiriki katika maamuzi mbalimbali ambayo yatawaletea ukombozi wao na taifa.
Hayo yamesemwa jijini
Dar-es-salaam na Mkurugenzi wa Chama cha Wanahabari Wanawake nchini (TAMWA)
Mama Edda Sanga alipokuwa akizungumzia mada kuhusu mapambano ya unyanyasaji na
ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake.
Mama Sanga alisema
kuwa unyanyasaji na ukatili dhidi ya wanawake kwa sasa umepungua kwasababu
chama chake kimefanya juhudi kubwa ya kuwaelimisha wananchi kuhusu kutoa
taarifa wanapoona kuna tatizo ili liweze kushughulikiwa mapema iwezekanavyo.
“Chama cha TAMWA
kimevitumia vyombo vya habari kutoa hamasa, kuelimisha na kufanya utafiti wa
kina kueleza ukatili huu, na hatimaye wahusika kufikishwa katika vyombo vya
dola” alisema Mama Sanga.
Aliendelea kusema
kuwa ingawa unyanyasaji na ukatili dhidi ya wanawake haujamalizika kabisa,
kumekuwepo kesi ambazo zinafikishwa mahakamani na hatua za kisheria
zinachukuliwa dhidi ya wanaofanya ukatili huo.
Mama Sanga alibainisha
mkoa wa Mara kuwa ndio mkoa sugu kwa unyanyasaji na ukatili wa wanawake. Alitoa
mfano wa Mama Neema Wandibe ambaye amefanyiwa ukatili wa kupindukia na
usiokubalika na mumewe hivi karibuni kwa kummwagia maji ya moto, kwasababu
alichuma mahindi mawili shambani na kuyachoma.
“Mkoa wa Mara
umekubuhu katika unyanyasaji kwasababu ya kufuata mila na desturi kandamizi,
ambazo zinamwona mwanamke kuwa ni mtu asiye na haki na sauti katika jamii”
alisema Mama Sanga.
Mama Sanga amewataka
wananchi na jamii kwa ujumla kushirikiana na vyombo husika katika kutoa taarifa
na kwamba wanahitaji kujenga jamii yenye malengo kwa ajili ya kuondoa madhara
ya unyanyasaji na ukatili wa wanawake.
Aidha, Mama Sanga
amewataka wanawake kujitambua, kujiamini na kutoa elimu kwa watoto wao ili
wakue katika hali ambayo ina umoja, na usawa katika kujiletea maendeleo yenye tija
na ustawi wa jamii bora.
Katika kuthamini na
kutambua mchango wa wanawake duniani Umoja wa Mataifa umetenga siku maalum ya
wanawake wote ambayo husherekewa tarehe 8, Machi kila mwaka.
Naye Katibu Mkuu wa
Wizara ya Afya, Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Bibi Sihaba Nkinga
alisema maadhimisho ya siku ya wanawake nchini yatafanyika katika ngazi ya
Mkoa.
Katibu Mkuu huyo
alisema kuwa maadhimisho ya mwaka huu yanaongozwa na kaulimbiu “Tanzania ya viwanda, wanawake ni msingi wa
mabadiliko ya kiuchumi”.
Zaidi ya hayo Katibu
Mkuu huyo aliendelea kusema kuwa kauli mbiu hiyo imeandaliwa kwa kuzingatia
mazingira ya Tanzania, vipaumbele vya kimaendeleo na dhamira ya dhati ya Serikali
ya Awamu ya Tano ya kufanya nchi kuwa ya viwanda na uchumi wa kati.

0 Comments