Subscribe Us

header ads

DKT.MABODI APOKELEWA KISHUJAA TUMBATU, ASEMA HAKUNA WA KUZUIA UTEKELEZAJI WA ILANI YA CCM Z'BAR.

 NAIBU KATIBU MKUU WA CCM Z’BAR DKT. ABDALLA JUMA SAADALA MABODI AKIWAPUNGIA MKONO WANANCHI NA WANACHAMA WA CHAMA HICHO MARA BAADA YA KUINGIA KATIKA MAKAAZI YA WANA TUMBATU GOMANI.
 KUNDI MAALUM LA VIJANA WA CHAMA HICHO WANAOTUMIA ZANA ZA ASILI KUSHEREHESHA WAKIONGOZA MSAFARA WA ZIARA HIYO KWA KUTOA BURUDANI  MBALI MBALI.
MAMIA YA WANACCM WALIOJITOKEZA KUMPOKEA NAIBU KATIBU MKUU WA CCM Z’BAR DKT. ABDALLA JUMA SAADALA MABODI  MARA BAADA YA KUWASILI KATIKA KISIWA HICHO.
MSAFARA WA NAIBU KATIBU MKUU WA CCM Z’BAR DKT. ABDALLA JUMA SAADALA MABODI  PAMOJA NA VIONGOZI,WANACHAMA NA WATENDAJI WA CCM WA KISIWA HICHO WAKIWA KATIKA ARDHI YA TUMBATU KUELEKEA KATIKA WADI YA TUMBATU GOMANI NDANI YA KISIWA HICHO.
NI NAIBU KATIBU MKUU WA CCM Z’BAR DKT. ABDALLA JUMA SAADALA MABODI  PAMOJA NA VIONGOZI  VIONGOZI WA MKOA WA KASKAZINI UNGUJA NA MAAFISA WA AFISI KUU ZANZIBAR WAKIWA KATIKA BANDARI NDOGO YA MKOKOTONI KUELEKEA KISIWA CHA TUMBATU KATIKA MWENDELEZO WA  ZIARA YA UIMARISHAJI WA HALI YA KISIASA YA  CCM KATIKA WILAYA YA KASKAZINI “A”.
NAIBU KATIBU MKUU WA CCM Z’BAR DKT. ABDALLA JUMA SAADALA MABODI AKIWAHUTUBIA NA KUWAPA NASAHA WANACHAMA WA CCM, VIONGOZI,   WATENDAJI WA JUMUIYA NA CHAMA WA NGAZI ZA MASHINA HADI MKOA KATIKA TAWI LA CCM GOMANI.

NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.

NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Dkt. Abdalla Juma Saadala Mabodi amesema kuwa hakuna Chama wala taasisi yoyote ya kisiasa inayoweza kuzuia Chama hicho kisisimamie utekelezaji wa  Ilani Uchaguzi ya mwaka 2015/2020 kwa wananchi wa Visiwa vya Zanzibar.

Msimamo huo ameutoa katika mwendelezo wa ziara zake za kuimarisha uhai wa Chama huko katika Kisiwa Cha Tumbatu Wilaya ya Kaskazini “A” kichama, wakati akizungumza na wanachama, viongozi na watendaji wa CCM Wadi ya Tumbatu Gomani.

Alisema kila jambo linalofanywa ama kutekelezwa na CCM lipo katika nyaraka za kimiongozo na kisheria ambazo ni Katiba ya Chama, Ilani na miongozo ya maadili na Uchaguzi tofauti na vyama vingine vya kisiasa vinavyoongozwa na matakwa binafsi ya watu wachache.

Pia alisema misingi hiyo ndio chimbuko la Ukomavu wa kisisa na Demokrasia iliyotukuka ndani ya  CCM, na inawajengea ujasiri viongozi wa chama hicho  kusimama popote kujenga hoja imara za kuinada ilani ya chama kwani wanajua kuwa hakuna wa kuzuia utekelezaji wake.

Mwanasiasa huyo ambaye amefanya ziara katika kisiwa hicho kidogo cha Tumbatu kilichopo Wilaya ya Kaskazini “A” Mkoa wa Kaskazini Unguja, kwa mara ya kwanza toka alipoteuliwa kushika nafasi hiyo hivi karibuni, aliwasihi Wana CCM hasa wazee kuendelea kuwa karibu na taasisi hiyo ili waweze kutoa ushauri na maoni yao juu ya masuala mbali mbali ya uongozi na utendaji.

Alieleza kwamba Chama hicho bado kinaendelea kutekeleza kwa vitendo ahadi zote zilizoahidiwa katika uchaguzi Mkuu uliopita bila ya kujali itikadi za kisiasa, kidini na kikabila  ili wananchi wote waweze kunufaika na matunda ya serikali inayotokana na Chama Tawala.

Dkt. Mabodi aliwambia wananchi hao kwamba wanatakiwa kuthamini na kulinda miradi mbali mbali inayotekelezwa na serikali kwani imetokana na nguvu zao ambao waliichagua kwa kura nyingi CCM isimamishe serikali yenye maono na utu wa kuwatumikia wananchi kwa vitendo.

Hata hivyo alifafanua kwamba CCM haina muda wa kurumbana na kushughulikia hoja dhaifu za wapinzani na badala yake inaenda mbio kusimamia kuwakumbusha viongozi na taasisi za umma zenye wajibu wa kushughulikia mipango ya maendeleo na ustawi wa jamii, kuona inakamilika kwa wakati.

“ CCM ni chama kinachotokana na ASP na TANU vilivyokuwa vyama vya wakulima na wakwezi na vikaikomboa nchi na kutuachia matunda haya, hivyo ni lazima tuyalinde na kuyatetea kwa vitendo.

Pia  puuzeni kwa nguvu zote uzushi na sera zizisokuwa na maana juu ya maisha na maendeleo ya nchi, kwani hazina lengo la kutufikisha pale tunapopataka zaidi ya kutugawa na ndio maana CCM inapinga kwa nguvu zote dhana za migogoro na utengano.”alieleza Dkt. Mabodi na kuwataka wana CCM kuendelea kulinda Amani na Utulivu wa nchi huku wakiendelea kufanya kazi kwa bidii za kujiongezea kipato.

Akitoa ufafanuzi juu ya Uchaguzi wa Chama hicho unaoendelea kwa ngazi ya Matawi kuchukua fomu aliwaagiza Makatibu na Manaibu Katibu wa Chama na jumuiya zingine kuahakikisha wanafuata taratibu zilizowekwa ili kila mtu mwenye nia ya kugombea apate nafasi hiyo.

“ Kama nikibaini kwamba kuna mizengwe ama makundi ya kutuharibia uchaguzi ngazi yeyote kwanza watu tuliowapa majukumu watawajibu pia uchaguzi huo nitawashauri wenzangu ikibidi ufutwe na kufanyika tena kwani tunahitaji watu wenye uwezo na uchungu na chama”. Alisema Naibu katibu huyo.

Aliwataka wanachama kuhakikisha wanachagua viongozi wenye sifa na wanaokubalika katika jamii ambao watajenga timu ya kukiletea ushindi na heshima chama hicho katika uchaguzi mkuu ujao.

Naye Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja, Haji Juma Haji akimkaribisha Naibu Katibu Mkuu huyo alisema kwamba CCM imepitia katika vipindi tofauti vya kiutawala hivyo bado ipo imara kutokana na uzoefu wake unaotokana na ridhaa halali za wananchi.

Mapema Katibu wa CCM  Wilaya ya Kaskazini “A” alisema kwamba  Serikali imeweza kutekeleza kwa ufanisi Ilani ya Uchaguzi ya Taasisi hiyo kwa vitendo kwani imeleza mageuzi makubwa ya kiuchumi  na kijamii, ambayo ni kuwapatia Umeme, vituo vya afya vya kisasa, skuli na miradi mbali mbali ya Uvuvi inayoharakisha maendeleo ya  wakaazi wa Tumbatu.

Aidha alilalamikia vyombo vya Ulinzi hasa Jeshi la Polisi ndani ya Wilaya hiyo kushindwa kutoa ushirikiano kwa viongozi wa CCM hasa pale wanapohujumiwa na watu wanaosadikiwa kuwa ni wapinzani.

Akizungumza mwanachama wa CCM wadi ya Tumbatu Bi. Nali Makame Ngwali alikishauri Chama hicho kuwapatia nafasi za kutembea sehemu mbali mbali nje ya kisiwa hicho kwa lengo la kwenda kutembea na kujifunza masuala mbali mbali hasa ya ujasiria mali na mafunzo ya kujiajiri wenyewe.

Wanachama wa CCM na wananchi wa Kisiwa hicho wamejitokeza kwa wingi kumpokea kwa shangwe kiongozi huyo toka alipotua katika Pwani ya kisiwa hicho.

Post a Comment

0 Comments