Subscribe Us

header ads

KAMPUNI YA TANZANITEONE YATOA MSAADA WA PRINTA MOJA NA KOMPYUTA MBILI KWA AJILI YA KITUOCHA POLISI MIRERANI

Mkuu wa kituo cha polisi Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, Evarest Makalla, akipokea printa kutoka kwa Ofisa mahusiano wa Kampuni ya TanzaniteOne, Halfan Hayesh ambapo makampuni hiyo ilitoa msaada wa printa moja na kompyuta mbili zenye thamani ya shilingi milioni 1.5 kwa ajili ya kusaidia kituo hicho.


Kampuni ya TanzaniteOne imetoa msaada wa kompyuta mbili na printa moja  kwa ajili ya kituo cha polisi Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara zitakazowasaidia kuandikia nyaraka na shughuli za polisi.

Msaada huo wenye thamani ya sh1.5 milion utawezesha askari polisi kuandika maelezo ya kazi, mambo ya utendaji na upelelezi wa kesi mbalimbali, tofauti na hapo awali walikuwa wanaenda mitaani kuandika kwenye ofisi binafsi za raia.
 
Ofisa mahusiano wa kampuni ya TanzaniteOne, Halfan Hayesh, akizungumza wakati akikabidhi msaada huo, alisema lengo lao ni kuwawezesha polisi ambao ni wadau wa usalama wa eneo hilo wanaofanya kazi kwa ukaribu.
 
Hayesh alisema wametoa kompyuta mbili mpakato (Lap top) aina ya Lenovo na print aina ya HP, ambazo zitawasaidia askari polisi kuweka kumbukumbu zao ipasavyo tofauti na hapo awali walipokuwa wanaenda kufanya kazi uraiani.
 
Alisema haikuwa jambo zuri kwa polisi kuandika kazi zao nje ya ofisi yao kwani inasababisha taarifa nyingi kujulikana au kuvuja kwa siri za kazi ila kupitia msaada huo tatizo hilo litakuwa limefikia ukingoni kupitia vifaa hivyo.
 
Mkuu wa kituo cha polisi Mirerani, mrakibu msaidizi wa polisi (ASP) Evarest Makalla akizungumza wakati akipokea msaada huo, alisema umetolewa wakati muafaka kwani utawasaidia kuweka usiri kwenye shughuli zao za kila siku.
 
Makalla alisema anaishukuru kampuni ya TanzaniteOne kwa kuwapa msaada wa vitendea kazi hivyo kwani baada ya yeye kufika kituoni hapo Julai 20 mwaka 2016 alibaini upungufu wa vifaa hivyo kwani kunasababisha uvujaji wa siri zao.
 
Alisema hiyo siyo mara ya kwanza kwa kampuni ya TanzaniteOne kutoa msaada kwa kituo cha polisi kwani wamekuwa wanawezesha misaada mingine ikiwemo kuweka mafuta kwenye magari ya polisi pindi wanapofanya shughuli za ulinzi.
 
“Kupitia nafasi hii naomba wadau wengine hasa wachimbaji wa madini ya Tanzanite wa vitalu vingine waige mfano huo kwa kusaidia kituo cha polisi ambacho kinaweka ulinzi kwa watu wote walipo eneo hilo.” alisema Makalla.
 
Alitoa ombi kwa kampuni hiyo ya TanzaniteOne kuendelea kutoa msaada kwenye kituo hicho kwani bado wana changamoto ya ukosefu wa pikipiki zitakazowawezesha kuendeleza ulinzi vizuri kwenye eneo hilo.
 
Meneja wa ulinzi wa kampuni ya TanzaniteOne, Abubakary Lombe alisema kampuni hiyo itaendelea kushirikiana na askari polisi wa kituo hicho kwani wamekuwa ni wadau wao wakubwa kwenye suala zima la ulinzi wa eneo hilo.
 
“Baada ya msaada huu wa vifaa vya ofisini, hatujafunga mlango wa kusaidiana kwani wote tunategemeana na pia suala la ulinzi ni mtambuka, hivyo tutaendelea kuwa pamoja kwa ajili ya faida yetu sote,” alisema Lombe.

Post a Comment

0 Comments