Subscribe Us

header ads

RC TARABA AMEWATAKA WANANCHI KUCHUKUA TAHADHARI NA NDEGE WAHARIBIFU WA MAZAO MASHAMBANI AINA YA KWELEA.

 Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Nyabaganga Taraba akiwasikiliza wakazi wa Kata ya Uchunga alipokwenda kufanya ziara na kuwatahadharisha kuhusu uvamizi wa ndege waharibifu wa mazao, kwelea kwelea.
 Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Nyabaganga Taraba (mwenye trakisuti ya bluu) akizungumza na watoto katika Shule ya Msingi Balele iliyopo Kata ya Mwadui Lohumbo alipokwenda kuwapa elimu kuhusu uaharibu wa ndege kwelea kwelea. Pembeni yake ni Mkuu Afisa Kilimo, Umwagiliaji na Ushirika, George Kessy.
 Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Nyabaganga Taraba akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Nyenze Kata ya Idukilo.
   Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Nyabaganga Taraba akiwapungia mikono wakulima waliokuwa wakiendelea na shughuli shambani katika Kata ya Mwadui Lohumbo.
Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Nyabaganga Taraba akizungumza na wananchi wa eneo la Utemini Kata ya Mwadui Lohumbo alipokuwa akiwatembelea na kuwatahadharisha kuhusu uvamizi wa ndege waharobifu mazao kwelea kwelea.

Na Mwandishi Maalumu, Kishapu

Mkuu wa Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga, Nyabaganga Taraba amewataka wananchi wilayani humo kuchukua tahadhari na baa la ndege waharibifu wa mazao mashambani aina ya kwelea.

Amesema tayari baadhi ya maeneo ya wilaya hiyo yamevamiwa na ndege hao waharibifu wa mazao yakiwemo ya mtama, uwele, alizeti na mahindi yanayoanza kustawi.

Taraba ambaye pia ni mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama alitoa tahadhari hiyo kwa wananchi mwishoni mwa wiki alipofanya ziara ya katika vijiji vya kata sita zilizopo wilayani humo.

Akiwa amembatana na Ofisa Kilimo, Ushirika na Umwagiliaji Wilaya, George Kessy na Ofisa Nyuki na Mkuu wa Jeshi la Polisi Wilaya (OCD), Emmanuel Gariyamoshi aliwatembelea wananchi wa kata za Uchunga, Mwadui Lohumbo, Idukilo, Ukenyenge, Mwamasele na Mwaweja.

Mkuu huyo wa wilaya aliwataka wananchi kulinda mashamba yao na kuwafukuza ndege hao wakati Serikali inaendelea kuchukua hatua za haraka ili kuwasaidia.
Alisema tayari wilaya imeagiza ndege maalumu kwa ajili ya kumwaga sumu kwenye mazalia ya ndege hao ili wasiongezeke na kuleta madhara zaidi kwa mashamba ya wananchi.

“Serikali haijawatupa nawaomba wananchi tukae mashambani mwetu tulinde na kuwafukuza ndege hao wasile mazao yetu kwani tutapata hasara kubwa, hatujui hao kwelea kwelea watakuja lini, na hatujui hiyo ndege itakuja lini,” alisisitiza.
Aidha, aliwataka wananchi kuvuna haraka iwezekanavyo mazao ambayo tayari yamekomaa ili kutowapa mwanya ndege hao kufanya uharibifu wao na hivyo kuwapa hasara wakulima.

Aliwataka wakulima wasihadaiwe na kuuza mazao yote kwa wafanyabiashara hali inayoweza kuwasababishia kukosa chakula baadaye na kulazimika kununua chakula kwa bei ya juu.

Aliwaonya watu wanaofanya hivyo kwani huwaacha nyuma wakulima waliotoka jasho kulima mazao wakati wao wakineemeka kwa kuyauza mazao hayo kwa bei ya juu na kupata faida.  

Kwa upande wake, Kessy alisema idara yake inawasisitizia wananchi wajenge utamaduni wa kuhifadhi chakula cha kutosha ghalani ili kiwasaidia katika siku zijazo na kuuza tu ile ziada inayobaki baada ya kutosheka.

Aliwapa mbinu za kufukuza kwelea kwelea kwa kuweka vitambaa mithili ya bendera, sanamu za watu na kupiga madebe ili kuwafukuza ndege hao ili wapiti mbali ya mashamba wasiweze kufanya uharibu.

Post a Comment

0 Comments