Benjamin Sawe Maelezo
TANZANIA kama ilivyo
nchi zingine duniani, imeshuhudia ukuaji wa sekta ya mawasiliano ambayo
imechangia katika kuboresha maisha ya wananchi kijamii na kiuchumi sambamba na
pato la taifa.
Ukuaji wa sekta hii
umechangiwa na kuwepo kwa sera, sheria kanuni na mfumo mzuri wa utoaji leseni
za huduma za mawasiliano.
Sekta
hii inachangia katika uchumi moja kwa moja na kwa kupitia sekta ya elimu, afya,
kilimo, biashara, ajira, mabenki, utalii, uwekezaji na sekta nyingine zote kama
nyenzo ya uwezeshaji katika kuongeza ufanisi wa utendaji kupitia jamii habari.
Takwimu
zinaonesha kuwa laini za simu zinazotumika zimeongezeka kutoka 34,251,801 mwaka
2014 hadi kufikia laini 39,808,419 mwaka 2015 na idadi ya watumiaji wa intaneti
waliongezeka kutoka 14,217,311 kwa mwaka 2014 hadi kufikia 17,263,523 kwa mwaka 2015.
Aidha,
zaidi ya asilimia 64 ya kaya nchini zinamiliki simu za mikononi. Pia ukuaji huu
umeongezeka hadi kwenye vituo vya kurusha matangazo.
Vituo
vya kurusha matangazo ya redio
vimeongezeka kutoka vituo 91 mwaka 2014 hadi kufikia vituo 116 mwaka 2015.
Wakati Tanganyika inapata uhuru mwak 1961 kulikuwepo na kituo kimoja cha redio
kwa sasa ni zaidi ya 140, kituo cha luninga hakikuwepo hata kimoja lakini miaka
55 baadae vipo zaidi ya 25.
Vilevile,
zaidi ya asilimia 79 ya teledensity/penetration
rate ambacho ni kiasi ambacho wananchi wamefikiwa na huduma za mawasiliano
ikiwemo ya simu, intaneti na utangazaji ambapo watoa huduma za mawasiliano ya
simu na posta pia wameongezeka na kuleta ushindani wenye tija na ufanisi nchini
kwa sekta zote.
Mafanikio
hayo yamewezesha kukua kwa kasi kwa sekta ya mawasiliano kutoka asilimia 8.0
mwaka 2014 hadi kufikia asilimia 12.1 mwaka 2015 na hivyo kuwa sekta ya kwanza
katika sekta za huduma na kuwa ya pili kwa sekta zote katika ukuaji hapa nchini.
Sekta
hii imechangia katika Pato Ghafi la Taifa kwa asilimia 3.6 mwaka 2015. Matokeo
haya ya ukuaji na mchango katika teknolojia ya habari na mawasiliano kwa sehemu
kubwa kumetokana na kuongezeka kwa matumizi ya huduma za mawasiliano zikiwemo
zile za muda wa maongezi kwa simu za viganjani na mezani, intaneti na
utangazaji.
Pia,
ufanisi huu umechangiwa na kukua kwa matumizi ya miamala ya kielektroniki
ambayo ni pamoja na uuzaji na ununuzi wa bidhaa na utoaji wa huduma kwa njia za
kielektroniki kama vile kutuma na kupokea pesa, kulipia ankara za maji, umeme,
ada, leseni za magari na usajili wa makampuni.
Utafiti
kupitia tathmini ya Global Microscope
umebaini kuwa Tanzania imeshika nafasi ya sita kati ya nchi 55 ulimwenguni na
inaongoza katika Bara la Afrika kwa kuwa na mazingira mazuri ya huduma za
kifedha kupitia simu za kiganjani.
Vilevile,
kwa mujibu wa ripoti ya Fiscope Survey
ya mwaka 2015, huduma za kifedha zimewafikia Watanzania kwa asilimia 76 kutoka
asilimia 44 mwaka 2009 ikiwa imechangiwa kwa kiasi kikubwa na uwepo wa Mawakala
wa Kibenki (Agent Bankings) pamoja na
huduma za kifedha kupitia makampuni ya simu kiasi cha kufikia akauti za miamala
ya kifedha (mobile money accounts)
kuwa 17,639,349 hadi Desemba 2015.
Tanzania
ni nchi ya kwanza duniani kwa kampuni za simu za viganjani kuwa na utayari na
makubaliano ya kutengamanisha (interoperability)
miamala ya huduma ya fedha.
Hii
imewezesha kupunguza gharama za kutuma fedha kutoka mtandao mmoja kwenda
mitandao mingine. Jambo hili limewezesha Tanzania kuongoza duniani katika
kutumia huduma ya Mobile Money Banking
kwa kiasi cha fedha zinazozunguka kwenye mtandao kwa wastani wa Shilingi
trilioni 4.5 kwa mwezi.
Ukuaji imara na wa kasi wa sekta ya
mawasiliano nchini ni sehemu ya matunda yanayoonekana na Serikali.Aidha Sera
nzuri za serikali na kufunguliwa kwa soko huria zimewezesha kuongezeka kwa
wawekezaji na hivyo kuwapa watumiaji fursa ya kuchagua huduma bora wanayohitaji
kwa gharama wanazomudu.
Katika kukabiliana na
changamoto ya idadi ndogo ya wananchi wanaotumia huduma za simu, Serikali
inaendelea kujenga mkongo wa taifa unaotarajiwa kufikia mikoa yote ili wananchi
wote waweze kutumia huduma ya intaneti kwa maendeleo yao.
Profesa Mbarawa
anasema wakati Serikali inaanza ujenzi wa mkongo huo ulikuwa umejengwa kiasi
cha kilometa 700 lakini hadi leo tayari ujenzi wake umefikia takribani kilometa
18,000.
“Nina uhakika baada ya
miaka miwili utakuwa umefikia zaidi ya kilometa 25, 000,” anasema. Anaeleza
kuwa Serikali inatambua umuhimu wa matumizi hayo ya simu nchini na ndio maana
imeanzisha huduma za kilimo mtandao, afya mtandao na elimu mtandao ili wananchi
na wao waweze kufanikisha mikakati ya kila sekta kupitia Teknolojia ya Habari
na Mawasiliano (Tehama).
Aidha, maendeleo ya
mkongo wa Taifa nchini Tanzania pia umesababisha kuongezeka kwa ukuaji wa
uchumi, kupunguza gharama za mawasiliano kutoka dola 20,000 za Kimarekani kwa
mwezi hadi dola 160 kwa mwezi, hilo likiwa ni punguzo la asilimia 99.
Pia imepunguza gharama
kwa watumiaji wa mwisho kutoka dola 0.06 kwa dakika mwaka 2009 hadi 0.03 dola
kwa dakika mwaka 2013 na pia kupunguza gharama za intaneti kutoka dola 16.45
kwa gigabyte moja mwaka 2009 hadi
dola 4.11 mwaka 2013.
Hayo ni kwa mujibu wa
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na, na Mawasiliano, Injinia Edwin Ngonyani
wakati wa uzinduzi wa Sera ya Mkongo wa Taifa mwaka 2016.
Bwana Ngonyani pia
anabainisha kuwa sekta ya TEHAMA ni moja ya nguzo muhimu katika ukuaji wa
uchumi wa taifa kwani ina mchango wa moja kwa moja na pia kwa sekta nyingine.
Wadau wengine
waliozungumza wakati wa uzinduzi huo waliipongeza serikali ya Tanzania kwa
hatua hiyo kubwa, wakisema itaongeza uwekezaji kwenye sekta ya hiyo nchini
humo.
Mshauri wa kiuchumi
kwenye Ubalozi wa Finland nchini humo Bwana Oskar Kass anasema upatikanaji wa
habari ni haki muhimu kwa raia wote, hivyo sera mpya inapaswa kuzingatia hilo.
Anaipongeza serikali
ya Tanzania kwa kusaidia sekta ya kibinafsi ili kuleta huduma za TEHAMA kwa
gharama nafuu na kuitaka sekta hiyo kusoma vyema sera mpya ili kujinufaisha na
fursa za uwekezaji zilizopo na zitakazoibuka.
Wakati tunapata Uhuru
kulikuwa hamna inteneti kipindi cha wakoloni simu zilitumiwa na wamissionari
pamoja na maeneo yenye vyombo vya ulinzi na usalama lakini leo kuna watanzania
zaidi ya milioni 20 wanaotumia simu za mkoni, kila ofisi ina simu za
ofisini,kuna inteneti kila jiji,miji na manispaa,kwa sasa mtoto wa miaka sita
anajua kutumia simu.
Ni ukweli usiopingika
kuwa sekta ya mawasiliano imekuwa kwa kasi katika ambapo inakadria kukua zaidi
ifikapo 2025. Ukuajia wa sekta hii unaenda sanjari na ukuajia wa uchumi kwani
mawasiliano bora na injini ya uchumi.

0 Comments