Random Posts

Manispaa ya Ubungo yamkabidhi mkandarasi kazi ya ujenzi wa daraja litakalogharimu mil.249,626,000

Mkurugenzi wa Manispaa ya Ubungo John L.Kayombo amemkabidhi mkandarasi  kazi ya kujenga daraja  ambalo lilibomoka na mvua na kusababisha kero kubwa kwa wananchi wa msumi kata ya Mbezi.
 Akiongea mbele ya wananchi wa Msumi  waliokuja kushuhudia makabidhiano hayo Mkurugenzi John L.Kayombo alisema amesikia kero hii ya daraja lililobomoka  muda mrefu takribani miaka 9 iliyopita kupitia mitandao na ndipo alipoamua kufuatilia kwa ajili ya kuona namna ya kutatua tatizo hilo ambapo baada ya kuona kero hiyo ni kubwa alichukua maamuzi ya kughairisha mradi mwingine ili gharama za pesa ile zitumike katika kutengeneza daraja hilo na kutatua kero hiyo kama ambavyo serikali imeahidi kuhakikisha inatatua kero za wananchi.
 Aidha amesema kuwa katika akaunti ya kata ya mbezi kuna kiasi cha Tshs mil 100 ambazo zitatumika kuanzia ujenzi wa daraja hilo mara moja na kuongeza kuwa kazi hiyo inaanza mara moja wiki ijayo kwa maana ya tarehe 1/10 /2017 na itachukua muda wa miezi 3 kukamilika.
 Alimtaka mkandarasi aliekabidhiwa kazi hiyo ambae nae alikuwepo eneo la tukio kufanya kazi hiyo kwa uaminifu na kwa utaalamu wa hali ya juu na ndani ya muda uliopangwa ili kuepuka matatizo yasiyo ya lazima kwani hatosita kumchukulia hatua za kisheria pamoja na kusitisha mkataba iwapo ataenda kinyume na taratibu.

Aliwataka pia wananchi kutoa ushirikiano kwa mkandarasi,meneja wa TARURA na injinia  ambao nao walikuwepo katika tukio hilo la makabidhiano.
 Baada ya hapo  aliwatambulisha meneja wa TARURA kwa manispaa ya Ubungo na timu yake na mkandarasi kwa wananchi.

Nae diwani wa kata ya mbezi Mh.Humphrey alimshukuru mkurugenzi kwa kuchukulia uzito suala hilo na kuamua  kulifanyia kazi kero ambayo imewasumbua  wananchi kwa muda mrefu.

Nae meneja wa TARURA ndugu Laynas Sanya alimshukuru Mkurugenzi na kuahidi kushirikiana bega kwa bega kuhakikisha kazi hiyo inafanyika kwa ufanisi.
Mkandarasi kampuni ya STEREO ESTATE alishukuru kwa makabidhiano hayo na kuahidi kuanza kazi mara moja wiki ijayo na kusema atazingatia yote aliyosisitizwa na Mkurugenzi.

Nao wananchi waliokuwepo kwenye eneo hilo walimshukuru mkurugenzi na kusema tatizo hilo limekuwa likiwasumbua kwa muda mrefu sasa takribani miaka 9 hivyo wana furaha sasa kuona amelichukulia uzito na kulifanyia kazi.

Daraja hilo litagharimu kiasi cha shilingi Mil 249,626,000 hadi kumalizika ujenzi wake ndani ya miezi 3.


IMETOLEWA NA KITENGO CHA HABARI NA MAHUSIANO- UBUNGO MUNICIPAL COUNCIL

Post a Comment

0 Comments