Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme
(TEMESA) Dkt. Mussa Mgwatu (kulia), akimuelekeza jambo Mkuu wa Kivuko cha
Magogoni-Kigamboni Mhandisi King’ombe Lukombe, wakati akikagua mashine za mfumo
wa kielektroniki wakukatia tiketi zitakazo wawezesha abiria wenye tiketi sahihi
kuingia kwenye jumba la abiria kwa ajili ya kusubiria vivuko.
Mkuu wa Kivuko cha Magogoni- Kigamboni Mhandisi
Kingómbe Lukombe (kushoto) akimuelekeza jambo Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi
na Umeme (TEMESA) wakati wa ukaguzi wa mradi wa uboreshaji mfumo wa mashine za
kielektroniki za kukatia tiketi, katika Kivuko cha Magogoni-Kigamboni.
Kibanda kipya cha kukatia tiketi kilichojengwa
katika kivuko cha Magogoni-Kigamboni upande wa Kigamboni, baada ya kubomolewa
kile cha awali, kilichokuwa karibu na jumba la kusubiria abiria, ili kupisha
mradi wa uboreshaji wa mfumo wa mashine za kielektroniki za kukatia tiketi na
baadae mradi wa upanuzi wa eneo hilo la abiria kusubiria vivuko.
Wafanyakazi wa Kivuko cha Magogoni- Kigamboni
wakimsikiliza Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) Dkt. Mussa
Mgwatu (aliesimama) alipofika kivukoni hapo kukagua mradi wa uboreshaji wa
mfumo wa kielektroniki wa kukatia tiketi na kupata fursa ya kuongea nao, baada ya
kumaliza mafunzo yao ya utoaji huduma bora kwa Mteja.
Picha na Theresia Mwami – TEMESA
.....
Na Theresia Mwami- TEMESA
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) Dkt. Mussa Mgwatu, ametembelea
na kukagua mradi wa maboresho ya mfumo wa kielektroniki wa kukatia tiketi
unaofanywa katika vivuko vya Magogoni-Kigamboni.
Mfumo huo utawezesha TEMESA
kudhibiti ukusanyaji wa mapato kwa kuhakikisha kuwa kila abiria analipa nauli
kamili kabla ya kupatiwa huduma ya kuvuka. Mradi huo umeigharimu TEMESA jumla
ya shilingi za kitanzania Bilioni 1.37 na unafanywa na kampuni ya Maxicom
Africa ya jijini Dar es Salaam.
Awamu ya pili ya Mradi itakuwa ni upanuzi wa
jumba la kusubiria abiria upande wa Kigamboni, mradi ambao tayari uko kwenye
hatua za ununuzi. Mradi wa kuboresha mfumo wa kukatia tiketi unatarajia
kukamilika mapema mwezi Oktoba, 2017.
Sambamba na ukaguzi wa mradi huo, Dkt. Mgwatu aliweza pia kuhudhuria
mafunzo ya awamu ya pili kuhusu utoaji huduma bora kwa wateja, yaliyokuwa
yakitolewa kwa watumishi wa kivuko hicho, na kuwataka watumishi waliohudhuria
mafunzo hayo kuzingatia uadilifu katika utendaji kazi wao wa kila siku pamoja
na kudumisha ushirikiano miongoni mwao ili kuweza kufikia malengo ambayo TEMESA
imejiwekea.
Watumishi waliokuwa wakipatiwa mafunzo hayo ni pamoja na wakaguzi
wa tiketi, mabaharia, mafundi wa vivuko, manahodha wa vivuko pamoja na
wakusanya mapato.
Nae Mkuu wa Kivuko cha Magogoni, Mhandisi King’ombe Lukombe aliwaambia
waandishi wa habari kuwa mafunzo hayo ya huduma bora kwa mteja (customer care)
yanatolewa kwa watumishi wote wa kivuko hicho, wakiwemo walinzi kutoka SUMA JKT
wanaotoa huduma ya ulinzi kivukoni hapo, lengo likiwa ni kuboresha zaidi huduma
kwa wateja wanaotumia huduma ya vivuko vya Magogoni-Kigamboni na kuondoa
malalamiko kwa watumiaji wa huduma hiyo.
Katika eneo la Magogoni, kuna jumla ya vivuko vitatu yaani MV. Magogoni,
MV. Kigamboni na MV. KAZI vinavyotoa huduma ya uvushaji wa abiria, magari na
mizigo na kwa wastani abiria zaidi ya elfu hamsini huvuka kwa kutumia vivuko
hivyo.




0 Comments