Random Posts

Viongozi wa Dunia Wavutiwa na Mageuzi ya Serikali ya Awamu ya Tano

  
Serikali ya Tanzania imepata heshima kubwa katika mkutano wa 72 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (UN) unaoendelea jijini New York nchini Marekani kutokana na kuenea kwa sifa za utendaji wa Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli.

Akizungumza kutoka New York anakomwakilisha Rais, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Augustine Mahiga amesema Tanzania imekuwa kivutio katika viunga vya UN kutokana na mtindo wa utendaji unaolenga kuwakomboa na kuwaletea huduma bora wananchi.

“Nimekutana na wajumbe kutoka nchi za Afrika, Asia, Ulaya na Marekani na wengi wanasema nchi zao ziko tayari kumualika Rais Magufuli au viongozi wao wako tayari kuja Tanzania kupata uzoefu jinsi Rais Magufuli anavyofanya mageuzi makubwa katika kipindi kifupi. Wanamuona ni mtu jasiri na mwenye upeo mkubwa katika kuwatumikia watu wake.

“Nchi hizi zinapishana kukutana na ujumbe wa Tanzania. Mpaka sasa, mbali na kuhutubia kwenye Baraza Kuu la UN, nimeshafanya mikutano ya nchi na nchi au na taasisi mbalimbali ipatayo 25 na wiki hii natarajia kufikisha mikutano 35,” anasema Waziri Mahiga.

Aidha kivutio kingine katika mkutano huo ni udogo wa ujumbe wa Tanzania. Mbali na Dkt. Mahiga ujumbe wake una maafisa wengine watatu tu kutoka Wizarani kwake wakiungana na Balozi wa Kudumu wa Tanzania kwenye Umoja wa Mataifa Balozi Modest Mero.

Akizungumzia ukubwa wa ujumbe aliouongoza, Waziri Mahiga anasema hii ni historia nyingine kwani katika mikutano ya UN, Tanzania imekuwa na ujumbe usiopungua watu 40 na wakati fulani walipata kufikia wajumbe 100; lakini sasa maafisa wachache wametekeleza kazi kwa ufanisi.

“Waandishi mbalimbali wa kimataifa walioko hapa pia wamekuwa wakifuatilia habari za idadi ya wajumbe na sisi pia walitufuata na kujua mpaka tulipofikia. Wameridhika na jinsi Tanzania inavyoenzi matumizi makini ya fedha za walipakodi,” aliongeza Waziri Mahiga.

Akihutubia Baraza Kuu, pamoja na kutoa salama maalum za Rais Magufuli, Waziri Mahiga amefafanua mageuzi mbalimbali yanayoendelea nchini hasa mapambano dhidi ya rushwa na kuimarisha uwajibikaji na akasisitiza utayari wa Tanzania kuendelea kushirikiana na UN.

Post a Comment

0 Comments