Mshambuliaji wa Young Africans ya Dar es Salaam, Obrey Chirwa
amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa Oktoba wa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL)
msimu wa 2017/2018.
Chirwa raia wa Zambia alitwaa tuzo hiyo baada ya kuwashinda wenzake
wawili, beki Erasto Nyoni wa Simba na mshambuliaji Ibrahim Ajibu pia wa
Young Africans alioingia nao fainali katika uchambuzi uliofanywa na
Kamati ya Tuzo za VPL zinazotolewa na Shirikisho la Mpira wa Miguu
Tanzania (TFF) kutokana na mapendekezo kutoka kwa makocha waliopo
viwanja mbalimbali ambavyo ligi hiyo inachezwa msimu huu.
Mshambuliaji huyo alitoa mchango mkubwa kwa Young Africans mwezi huo
ikipata pointi saba katika michezo mitatu iliyocheza na kupanda katika
msimamo wa ligi kutoka nafasi ya sita iliyokuwepo mwezi Septemba hadi ya
pili mwishoni mwa Oktoba.
Young Africans iliifunga Kagera Sugar mabao 2-1 Uwanja wa Kaitaba,
Bukoba, ambapo Chirwa alifunga bao moja na kutoa pasi ya mwisho ya bao
moja, pia Yanga iliifunga Stand United mabao 4-0 Uwanja wa Kambarage,
Shinyanga, ambapo Chirwa alifunga bao moja na kutoa pasi ya mwisho ya
bao moja.
Kiwango cha mchezaji huyo kilionekana pia katika mchezo wa watani wa
jadi Yanga na Simba uliofanyika Oktoba 28, 2017 Uwanja wa Uhuru, Dar es
Salaam na kumalizika kwa sare ya bao 1-1. Bao la Yanga lilifungwa na
Chirwa, hivyo kwa mwezi huo alifanikiwa kuwa na kiwango cha juu katika
kila mchezo ikiwa ni pamoja na kufunga.
Kwa upande wa Erasto naye alitoa mchango mkubwa kwa Simba uliowezesha
timu hiyo kupata pointi nane katika michezo minne iliyocheza, akitoa
pasi za mwisho za mabao nne, ambapo Simba ilishinda michezo miwili na
kutoka sare miwili, huku Ajibu akitoa mchango mkubwa kwa Yanga ikiwa ni
pamoja na kufunga mabao matatu na kutoa pasi ya mwisho ya bao moja.
Wachezaji wengine ambao tayari wameshinda Tuzo ya Mchezaji Bora wa
mwezi wa VPL msimu huu ni mshambuliaji wa Simba, Emmanuel Okwi (Agosti),
beki wa Singida United, Shafiq Batambuze (Septemba).
Kampuni ya Vodacom, ambao ndiyo wadhamini wa ligi hiyo ina utaratibu
wa kuwazadiwa wachezaji bora wa kila mwezi, huku pia mwisho wa msimu
kukiwa na tuzo mbalimbali zinazohusu ligi hiyo, ambapo msimu wa mwaka
2016/2017 kulikuwa tuzo 16 zilitolewa kwa washindi wa kada
mbalimbali. Chirwa atazawadiwa Sh milioni moja kwa kuibuka Mchezaji Bora
wa Oktoba.

0 Comments