…
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa
amewataka wakulima wa ufuta katika mikoa inayolima zao hilo nchini kuuza
kwa kutumia njia ya minada na si mashambani.
Ametoa agizo hilo leo (Jumamosi,
Machi 03, 2018) wakati akizungumza kwa nyakati tofauti na wananchi wa
vijiji vya Nachihungo, Narungombe na Chikwale.
Waziri Mkuu ambaye yuko wilayani
Ruangwa kwa ziara ya kikazi amesema ili wakulima waweze kupata tija ni
vema wakauza ufuta wao kwa kupitia minada kama inavyofanyika katika zao
la korosho
“Usikubali kumuuzia mtu yeyote
ufuta wako ukiwa shambani kwa sababu bei atakayonunulia ni ndogo
kulinganisha na soko, naamini ufuta wote ukiuzwa katika minada mtaona
faida.”
Kufuatia agizo hilo amemuagiza
Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Ruangwa, Bw. Andrea Chezue aandae
utaratibu wa maeneo ya kukusanyia ufuta na kufanyia minada.
Amesema ufuta unaolimwa nchini ni
bora na unapendwa sana duniani hivyo wasiwe na wasiwasi. Baadhi ya Mikoa
inayolima ufuta kwa wingi ni Lindi, Pwani, Dodoma, Manyara, Kigoma na
Singida.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu
amesema vijiji vote visivyokuwa na umeme nchini vikiwemo vya wilaya ya
Ruangwa vitaunganishiwa katika REA awamu ya tatu.
Amesema wananchi waendelee kuwa na
subira kwa sababu tayari mkandarasi ameshaanza kazi ya kuunganisha
umeme katika vijiji vingine vya wilaya hiyo na atafika kwenye maeneo
yao.
Alibainisha kuwa mkakati wa Rais
Dkt. John Magufuli ni kuhakikisha wananchi wote nchini waunganishiwa
nishati ya umeme kwenye majumba yao, hivyo waendelee kuwa na subira na
kushirikiana na Serikali yao.
Kuhusu suala la upatikanaji wa
huduma ya maji safi na salama alisema, “Huduma ya upatikanaji wa maji
safi na salama kwa wananchi ni miongoni mwa vipaumbele vya Serikali ya
Awamu ya Tano, hivyo vijiji vyote vitapata maji”.
Pia alitumia fursa hiyo
kuwahamasisha wananchi kote nchini kutunza vyanzo vya maji ili
kuliepusha taifa kugeuka jangwa pia miradi inayoletwa na Serikali iwe
endelevu

0 Comments