Random Posts

Mshama Awatembelea Waliokumbwa na Adha Iliyotokonana na Mvua Kitongoji cha Janga

 Mkuu wa wilaya ya Kibaha Assumpter Mshama, akizungumza na wakazi waliokumbwa na adha ya nyumba zao kuzungukwa na maji yaliyotokana na mvua zilizonyesha siku tatu mfululizo,kitongoji cha Janga kata ya Janga.(Picha na Mwamvua Mwinyi)
 Baadhi ya nyumba  zilizozungukwa na maji yaliyotokana na mvua zilizonyesha siku tatu mfululizo,kitongoji cha Janga kata ya Janga.(Picha na Mwamvua Mwinyi)
Na Mwamvua Mwinyi,Kibaha

NYUMBA zaidi ya 30 zilizoko kwenye Kitongoji cha Janga, kata ya Janga wilaya ya Kibaha ,mkoani Pwani zimezungukwa na maji, hali iliyosababisha wenye nyumba hizo kuhama kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha mfululizo.

Akizungumza na wakazi waliokumbwa na adha hiyo ,mkuu wa wilaya ya Kibaha Assumpter Mshama alisema wale ambao nyumba zao zipo jirani na bonde ,na zinaanza kuingiliwa na maji waondoke kabla hayajaleta madhara .

Aidha alieleza wale ambao nyumba zao zilizo ndani ya maji watapewa viwanja bure.
"Mlioko kwenye nyumba zaidi ya 30 zilizo kwenye maji na zinazokaribia kuingiliwa na maji muondoke ili kuepukana na madhara yanayoweza kujitokeza ikiwa ni pamoja na kupoteza maisha" alisisitiza.

Assumpter alieleza, wakazi hao walijenga nyumba kwenye eneo hilo ambalo zamani kulikuwa na bonde ambalo lilikuwa linalimwa mpunga  na kuchimbwa kisima kwa ajili ya maji.

"Gharama za kutaka kujenga mfereji ni kubwa sana na serikali haina fedha za kufanya hivyo njia pekee ni wakazi kuhama ili kuepusha maafa yanayoweza kujitokeza kwani eneo hili halifai kuishi," 

"Ambao nyumba ziko ndani ya maji watapatiwa viwanja bure sehemu nyingine lakini watajenga wenyewe ,hawapaswi kuwepo hapo tena kwani hapafai kuishi"

"Kwanza hapa hamna hati za ujenzi wala za eneo hili na hapa hapajapimwa kwa hiyo hapa so sehemu sahihi ya kuishi kwani maeneo yote yamepimwa laki hapa hapajapimwa hivyo in vema mkaondoka," alifafanua Assumpter.

Diwani wa kata ya Janga, Chande Muhalika alisema ni tukio la kwanza kutokea kwenye bonde hilo .

Kwa mujibu wa diwani huyo ,zamani maji yalikuwa kidogo sana lakini safari hii maji yamekuwa mengi .

Nae ofisa mtendaji wa Mji Mdogo wa Mlandizi Michael Mwakamo alisema kuwa ,baada ya kutokea hali hiyo waliwataka wananchi hao kuondoka ili kuepusha madhara ambapo walioondoka na hakuna mwananchi aliyedhurika.

Nao baadhi ya wakazi waliokumbwa na janga hilo ,akiwemo  Luteni Kanali mstaafu wa Jeshi Angolile Mwakajinga, Ramadhan Hemed,  Sophia Matitu walifafanua baada ya kuona maji yanaongezeka waliomba jeshini kambi ya Ruvu Jkt mashine kwa ajili ya kuvutia maji lakini hawakufanikiwa.

Walibainisha waliongea na wataalamu wa Halmashauri ya wilaya ya Kibaha juu ya uwezekano wa kuyatoa maji hayo wakasema njia pekee ni kuchimba mtaro mkubwa na kuyapeleka maji hayo mto Mkalamo .

Hata hivyo gharama za kufanya hivyo zikaonekana kuwa kubwa.

Post a Comment

0 Comments