Naibu Waziri wa
Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akihutubia wananchi wa kata
ya Busunzu iliyopo jimboni kwake Muhambwe wilayani Kibondo mkoani Kigoma wakati
akikagua maendeleo ye ujenzi wa kituo cha afya cha kata hiyo baada ya kushiriki
mbio za mwenge wa uhuru wa kitaifa wilayani humo mkoani Kigoma
Muonekano wa kifaa cha
umeme cha kampuni ya Solkit iliyopigwa marufuku na Naibu Waziri wa Uchukuzi na
Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye kusambaza umeme kwa gharama kubwa kwa
wananchi wa jimboni kwake Muhambwe wilayani Kibondo mkoani Kigoma
Naibu Waziri wa
Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akikagua maendeleo ya ujenzi
wa choo cha wanafunzi wa shule ya Sekondari ya Misezero ambapo aliwapatia
sementi kwa ujenzi wa choo hicho kilichopo jimboni kwake Muhambwe wilayani
Kibondo mkoani Kigoma
Naibu Waziri wa
Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akiwapongeza wanafunzi wa
shule ya sekondari ya Olivegreen iliyopo kwenye jimbo lake la Muhambwe wilayani
Kibondo, Kigoma kwa ufaulu mzuri katika ngazi ya mkoa na hivyo wilaya hiyo
kuongoza kitaifa
Naibu Waziri wa
Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akikagua maendeleo ya
ukarabati wa bweni la wanafunzi wa shule ya sekondari ya kiislamu ya Kakangaga
baada ya kuunga na moto ambapo amewapatia mifuko ya sementi 20 na mabati 24 iliyopo
jimboni kwake Muhambwe wilayani Kibondo mkoani Kigoma
.........................................................
Naibu Waziri wa
Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye amepiga marufuku kampuni ya
Solkit inayosambaza na kuuza vifaa vya umeme wa jua kwa wananchi wa jimbo la
Muhambwe lililopo wilayani Kibondo mkoani Kigoma
Nditiye amesema hayo
akiwa kwenye ziara jimboni kwake Muhambwe wakati akiwahutubia wananchi
alipofika kukagua maendeleo ya ujenzi wa kituo cha afya cha Busunzu kilichopo
Wilayani Kibondo mkoani Kigoma. Aliwasili Wiayani humo wakati wa mbio za Mwenge
wa Uhuru za kitaifa kwenye Wilaya hiyo ambapo alijumuika na wananchi wake
kukimbiza Mwenge na kukagua na kuzindua miradi mbali mbali ya maendeleo
Wilayani humo.
Amesema kuwa Kampuni
ya Solkit ni kampuni binafsi inayouza na kusambaza vifaa vya umeme wa jua kwa
wananchi wa jimbo lake hilo kwa gharama kubwa ambazo ziko nje ya uwezo wa
wananchi kwa kuingia nao mikataba ya utata isiyokuwa na uwazi ambayo inawataka
wananchi walipie kiasi cha shilingi 38,000 kwa ajili ya kununua vifaa vya
kampuni hiyo na kuendelea kulipia shilingi mia saba kwa siku kwa kipindi cha
mwaka mzima kwa muda wa miaka mitatu.
Amefafanua kuwa
kiwango hicho ni kikubwa kwa wananchi wa jimbo lake ukilinganisha na gharama
nafuu zinazotozwa na taasisi ya Serikali inayohusika kusambaza umeme vijijini,
taasisi ya REA ambapo mwananchi anaweza kulipa kiasi cha shilingi elfu tatu
hadi tano tu kwa mwezi ambapo gharama za kampuni ya Solkit zipo nje ya uwezo wa
kiuchumi wa kaya husika na fedha wanazotumia kununua umeme wa kampuni hiyo zingeweza
kutumika kuipatia familia husika mahitaji mengine ya kijamii na kiuchumi.
Amewaeleza wananchi wa
jimbo lake kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya uongozi wa
Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli ina lengo na dhamira ya dhati ya kuwapatia
wananchi umeme wa gharama nafuu kupitia taasisi ya Serikali ya REA inayosambaza
umeme vijijini.
“Wananchi tumeshuhudia uzinduzi wa Awamu ya Tatu ya umeme wa
REA ikifanyika kwenye kata yetu ya Mabamba ambapo ulifanywa na Waziri wa
Nishati Dkt. Medard Kalemani, hizi zote ni jitihada za Serikali yetu
kuhakikisha kuwa kila mwananchi anapata umeme ili kutekeleza majukumu yake,
kuendesha shughuli za kiuchumi na kijamii ambazo zitawawezesha kuongeza kipato
cha familia na taifa kwa ujumla” amesema Nditiye.
Naye Mwenyekiti wa Kijiji
cha Busunzu Bwana Zacharia Mbumba alimshukuru Nditiye kwa kupiga marufuku
Kampuni ya Solkit kwenye Wilaya ya Kibondo kwa kuwa gharama za ununuzi na
malipo ya umeme wa kampuni hiyo kwa siku kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo
ni kubwa ukilinganisha na gharama za umeme wa vijijini unaotelwa na Serikali kupitia
REA pamoja na hali ya kipato cha mwanakijiji.
Pia Ameongeza kuwa
wanakijiji wameitikia wito wa kuchangia asilimia 20 za gharama za ujenzi wa
kituo cha afya cha kata ya Busunzu ili kuboresha utoaji wa huduma za afya kwa
wananchi ambapo kituo hicho kinahitaji jumla ya shilingi milioni 133 ili ujenzi
wake uweze kukamilika ambapo wananchi wanatarajia kuchangia shilingi milioni 13
na tayari wamekusanya kiasi cha shilingi milioni mbili na wananchi
wamekubaliana kuchangia shilingi elfu mbili kwa kila mmoja kwa mwananchi
aliyefikisha umri kati ya miaka 18 hadi 59.
Mwenyekiti wa CCM wa
Kata ya Busunzu Bwana Gilesi Kagoma amesema kuwa, “ujenzi wa kituo cha afya
inatuhusu wote na haichagui huyu wa CCM au CHADEMA kwa kuwa sote ni wanufaika
na kituo kikikamilika tutanufaika wote,” amesema.
Aidha, Nditiye ambaye pia ni
Mbunge wa jimbo la Muhambwe ambapo kituo hicho cha afya kipo ndani ya jimbo
hilo amechangia mifuko mia moja ya sementi kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho
na amewaahidi kuendelea kuchangia kadri ujenzi unavyoendelea. Pia, amewapongeza
wananchi kwa walivyojitoa na kuchangia ujenzi wa kituo hicho.
Nditiye pia amefanya
ziara ya kukagua maendeleo ya shule za sekondari za Misezero na Olivegreen
ambapo amechangia mifuko ya sementi, kompyuta, vitabu vya waalimu kwa ajili ya
kufundishia, matengenezo ya barabara zinaingia shuleni, kufikisha umeme kwenye
majengo ya shule, kukagua ujenzi wa miundombinu ya madarasa na vyoo ambapo
alitoa sementi kwa ajili hiyo na kukaguabweni la shule ya sekondari ya
Kakangaga iliyoungua na moto ambapo amewapatia mifuko 20 ya sementi, mabati 24
na kompyuta mbili ili kukamilisha ujenzi wa bweni hilo.
Imetolewa
na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini,
Wizara
ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
0 Comments