Subscribe Us

header ads

Mkoani Pwani Wahimizwa Kulima Pamba ili Kujiinua Kiuchumi

Mkuu wa mkoa wa Pwani mhandisi Evarist Ndikilo, wakati alipotembelea shamba la pamba la mzee Rashid Msilu huko Chalinze, Bagamoyo ambapo alihimiza wakulima Mkoani humo kulima zao hilo .(Picha na Mwamvua Mwinyi)

Na Mwamvua Mwinyi, Bagamoyo

WAKULIMA wa mazao ya kibiashara Mkoani Pwani, wamehamasishwa kulima kilimo cha pamba ili kujiinua kimaendeleo na uchumi .

Aidha imekemea utoaji wa dawa za viuadudu vinavyoshambulia zao hilo ambazo ni feki na kudai mtu atakaegawa dawa feki  ,atachukuliwa hatua kali ,kwani inasababisha kudididimiza juhudi za wakulima hao.

Mkuu wa mkoa wa Pwani ,mhandisi Evarist Ndikilo alihimiza kilimo hicho, wakati alipokwenda kutembelea shamba la pamba la mzee Rashid Msilu huko Kweikonje ,Bagamoyo.

Alisema katika mkoa huo maeneo yanayostawi zaidi kilimo cha pamba ni wilaya ya Rufiji na Chalinze.

Ndikilo alieleza, kipindi cha nyuma kilimo hicho kilitetereka lakini kwasasa mazingira na ardhi inaruhusu kuinua kilimo cha zao hilo.

Kwa mujibu wa mkuu huyo wa mkoa, kupitia wizara ya kilimo imeshasambaza mbegu bora ya pamba,mabomba ya kupulizia dawa kwa mkopo na dawa za viuadudu zimetolewa bure.

Ndikilo alifafanua, Chalinze imeshapatiwa lita 226 za dawa za kupulizia kuzuia wadudu waharibifu ,Rufiji imepewa lita 120 ambapo mabomba ya kupulizia dawa yametolewa 40 kwa ajili ya Chalinze na Rufiji mabomba kumi.

Aliomba dawa hizo ziwafikie wakulima wa pamba ili kuleta tija.

"Kuhusu dawa feki ,nimesikia kwa baadhi ya wakulima kuwa mwaka jana zililetwa dawa feki ,hazikuuwa wadudu,kwakweli kipindi hiki sitokubali kusikia tatizo hilo tena" alisisitiza Ndikilo.

Pamoja na hayo , alikemea pasiwepo na hujuma yeyote wakati wa hatua ya uvunaji .

"Kuna baadhi ya wakulima wanaweka maji ,mawe ,mchanga kwa lengo la kuongeza uzito ,;msifanye hivyo mnashusha sifa ya mkoa na Taifa ".

Ndikilo alisema  pia, vyama vya msingi viwe na maghala ,mizani halali na vifungashio bora ili kupeleka vyama vya ushirika kupata masoko ya uhakika.

Alielezea mwaka jana alisikia chama cha ushirika -Corecu hakikuchukua pamba za wakulima kutokana na kukosa fedha ,hivyo aliwahakikishia wakulima ataongea na mwenyekiti wa Corecu kuangalia namna ya kununua pamba hizo .

Nae ofisa Kilimo,Umwagiliaji na Ushirika Chalinze Jovin Bararata ,alisema halmshauri ya Chalinze ni moja ya halmshauri zinazolima pamba Mkoani hapo .

Alibainisha, mwaka jana walivuna tani 63 na mavuno yajayo wanatarajia kuvuna tani 250.

Bararata alielezea ,wamejiwekea mikakati ya kuhamasisha kilimo hicho ambapo wamenunua pikipiki 15 ambazo watagawiwa maafisa ugani ili waweze kuwatembelea wakulima mbalimbali kirahisi .

Mkakati mwingine ni kukabiliana na tatizo la soko kwa kuimarisha vyama vya msingi ili kuhakikisha vinaratibu vizuri na kukusanya pamba":, wakulima waweze kunufaika na mfumo wa stakabadhi ghalani.

Bararata alisema ,ipo changamoto ya wadudu waharibifu na panya ambapo wanadhibiti hali hiyo kwa kushirikiana na bodi ya pamba kwa kuhakikisha dawa zinagawiwa kwa wakati.

Mkulima wa pamba , mzee Rashid Msilu aliishukuru serikali kwa kuwapatia dawa,mbegu bora ili kulima kisasa.

Nchi ya Tanzania inaingiza fedha nyingi za kigeni kwa mazao ya biashara makubwa matano ikiwemo kahawa, chai, korosho,pamba na Tumbaku lakini zao linaloongoza kuingiza fedha hizo ni korosho.

Kwa mkoa wa Pwani ,zao la biashara linaloingiza fedha za kigeni ni korosho ambapo kwasasa serikali Mkoani humo inahimiza pamba ili kuwa na mazao mawili ya kibiashara.

Post a Comment

0 Comments