Subscribe Us

header ads

Gereza la Kilimo Mollo lapongezwa


Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkrikiti akikabidhi funguo ya nyumba kwa askari B1632 S'SGT Jabil Mohamed  Mkwazu akiwa na mkewe (kushoto) wakati wa hafla iliyofanyika Gereza Mollo Sumbawanga mwishoni mwa wiki.
Mkuu wa Gereza la Kilimo Mollo SP Nicostratus Magori akitoa taarifa ya miradi ya gereza kwa Mkuu wa Mkoa (hayupo pichani) wakati wa hafla ya ufunguzi mradi wa nyumba bora za kuishi askari.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti akikata utepe kuashiria uzinduzi wa nyumba mpya ya kuishi askari kwenye Gereza Moro wilaya ya Sumbawanga. Kulia ni Mkuu wa Magereza Mkoa wa Rukwa ACP Motrais Mwakiluma na kushoto ni Mkuu wa Gereza  Mollo SP Nicostratus Magori.

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti (wa pili toka kushoto) akiwasili Gereza la Kilimo Mollo wilayani Sumbawanga kwa ziara ya kuzindua miradi ya maendeleo juzi.


 Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti akifungua koki ya maji kuashiria uzinduzi wa mradi wa maji safai na salama juzi kwenye Gereza la Kilimo Mollo wilaya ya Sumbawanga.

(Habari na Picha na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Rukwa)


Jeshi la Magereza nchini limepongezwa kwa kubuni utaratibu mzuri wa kujiendesha kimapato kupitia miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa nyumba bora kwa gharama nafuu.

Pongezi hizo zimetolewa mwishoni mwa wiki na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti, wakati akizindua mradi wa nyumba za kuishi askari na mradi wa maji kwenye Gereza la Kilimo Mollo Wilaya ya Sumbawanga.

Mkirikiti alifurahishwa kuona mradi wa nyumba ya kuishi familia mbili iliyojengwa kwa sh. mil 55 na aliwapongeza kwa kutekeleza dhana ya Magereza ya kujigemea kwakuwa inaongeza tija kwa Mkoa kupitia miradi inayotekelezwa.

“Kama Magereza imeweza kujenga nyumba moja ya famili kwa gharama ya sh mil 57, huu ni mfano mzuri wa ubunifu. Wito wangu kwa Halmashauri za Rukwa ziige mfano huu kwenye utekelezaji miradi ya ujenzi ili kupunguza gharama za fedha za Serikali “alisisitiza.

Awali akitoa taarifa ya miradi, Mkuu wa Gereza la Kilimo Mollo,Mrakibu wa Magereza (SP) Nicostratus Magori, alisema mradi wa nyumba za kuishi askari umetekelezwa kwa lengo la kupunguza uhaba wa makazi bora ya askari .

Aliongeza kusema gharama halisi za mradi wa nyumba hiyo ni sh. mil 55 ambapo gereza kupitia miradi yake limechangia sh. mil 17.3 na Kamishna Jenerali wa Magereza (CGP) alichangia sh. mil 38.

Kuhusu mradi wa maji safi na salama SP Magori alisema shil mil  7.6 imetumika kufufua mradi huo ambapo fedha zote zimetokana na miradi ya Gereza la Mollo.

SP Magori alitoa ombi kwa Mkuu wa Mkoa kuwa Gereza lisaidie kupata miradi mbalimbali kwa kuwa lina nguvu kazi na utaalam, hatua itakayosaidia kutekeleza miradi kwa ubora huku gereza likiongeza uwezo wake wa kujitegemea kimapato.

“Miradi hii licha ya kutuimarisha kiuchumi, inasaidia pia kutoa mafunzo ya ujuzi kwa wafungwa ili watakapomaliza vifungo vyao itawasaidia kuwa raia wema kwa kufanya kazi halali za kujitegemea” alisema SP Magori.

Gereza la Kilimo Mollo lilianzishwa mwaka 1967 na lina eneo la ekari  8,989 na kwa sasa lina miradi ya ujenzi wa nyumba ya kulala wageni, ujenzi wa bwalo, ujenzi wa fremu 11 za maduka na ujenzi wa viwanda vidogo vya kuchakata mazao ya ngano, alizeti na mahindi.

Post a Comment

0 Comments