Monday 30 October 2023

Dk.Mahenge awataka wawekezaji kujisali TIC, ili wapate manufaa

Mjiolojia Mwandamizi wa Mgodi wa Uchimbaji Madini wa Shanta, uliopo Wilaya ya Ikungi mkoani Singida, Sijali Mhozya (kulia) akielezea jinsi mgoni huo ulivyo mbele ya Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) Dk. Binilith Mahenge (katikati) alipoutembelea mgodi huo Oktoba 28, 2023.
Mwenyekiti  wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) Dk. Binilith Mahenge, akizungumza na viongozi wa mgodi huo.
Kaimu Meneja wa mgodi huo, Reuben Ngusaru akizungumza kwenye kikao hicho.
Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa TIC, Mhandisi Peter Chisawillo, akizungumza.
Meneja wa TIC Kanda ya Kati Venance Mashiba, akizungumza katika mkutano na wawekezaji wa Mkoa wa Singida uliofanyika Hoteli ya KBH
Picha ya pamoja na wafanyakazi wa mgodi wa Shanta
Kaimu Katibu Tawala Msaidizi sehemu ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida, Lucas Mkuki, akizungumza.
Mwakilishi wa Kiwanda cha kusindika mafuta cha Wild Flower,Grains and Oil Mill Project, Jamal Juma, akichangia jambo kwenye mkutano wa wakezaji Mkoa wa Singida.
Picha ya pamoja na wawekezaji wa Mkoa wa Singida.
Muonekano wa eneo la uchimbaji wa mawe yenye dhahabu.
Muonekano wa bwawa linalohifadhi maji yenye kemikali kutoka katika mgodi huo.
Muonekano wa moja ya mitambo ya kuchenjua dhahabu katika mgodi huo.
....................................

Na Dotto Mwaibale, Singida

MWENYEKITI wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) Dk. Binilith Mahenge ameendelea kuwahimiza wawekezaji kusajili kazi zao za biashara wanazozifanya ili waweze kutambulika na kupata fursa mbalimbali.

Dk.Mahenge ametoa ombi hilo kwa nyakati tofauti alipokuwa akizungumza na viongozi wa mgodi wa uchimbaji madini wa Shanta uliopo Wilaya ya Ikungi na baadhi ya wawekezaji wa Mkoa wa Singida alipokuwa kwenye ziara yake ya kikazi ya kampeni ya kuhamasisha uwekezaji, kukutana na wawekezaji na kujua changamoto walizonazo ili kuzitafutia ufumbuzi.

Alisema hivi sasa suala la uwekezaji ni la muhimu si kwa Tanzania peke yake bali kwa dunia nzima ambapo katika kila nchi kumekuwa na makongamano yakifanyika ya kutangaza fursa mbalimbali za uwekezaji.

"Uwekezaji hivi sasa kila mahali pote duniani ni ushindani ukienda uchina, Marekani, Urusi, India wanataka wawekezaji na kila wiki makongamano yanafanyika kwa ajili ya kutangaza vivutio walivyo navyo ili kutafuta wawekezaji ni jambo ambalo tunanyang'anyana," alisema Dk.Mahenge.

Alisema Rais Dkt. Samia Suluhu tulimsikia aliposema Serikali peke yake haiwezi kuleta maendeleo katika nchi ni lazima ishirikiane na sekta binafsi ambapo wanapatikana wawekezaji.

Alisema TIC wamepewa dhamana na Serikali ya kuhamasisha uwekezaji pamoja na kuusajili kutokana na umuhimu huo ndio maana wanafanya ziara ya kuwatembelea kuona kazi wanazozifanya, kujua changamoto zao na kuwahamasisha wazisajili.

Alisema TIC imeanzisha kampeni ya kuhamasisha wawekezaji wa ndani kujisajili na kujulikana ili nao wapate faida kama wanayoipata wawekezaji wengine kutoka nje ya nchi kwani wengi wao hawajasajiliwa na wengine hawajulikani kabisa.

Kaimu Meneja wa mgodi wa uchimbaji wa madini wa Shanta Reuben Ngusaru akizungumza katika kikao na Mwenyekiti huyo na ujumbe wake alisema moja ya changamoto kubwa walionayo ni ukatikaji wa umeme mara kwa mara hivyo kufifisha utendaji wa kazi kwa ufanisi na uzalishaji.

“Tuna jenereta letu lakini tukiliwasha kwa masaa 12 ni sawa sawa na kutumia umeme wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa siku sita hiyo ni gharama ya mafuta na hivi sasa tupo kwenye mgao wakati mwingine tunakuwa kwenye mgawo huo kwa saa 12 na hii robo ya mwaka ya nne hata maduhuli yatapungua na hii ni changamoto kubwa sana kwetu,” alisema Ngusaru.

Ngusaru alitaja changamoto nyingine ya kisheria ni suala la sera mpya ya Serikali ya kubakisha asilimia 40 ya fedha katika Kata ya Mang’onyi ulipo mgodi na asilimia 60 kupelekwa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi.

Alisema kiwango hicho ni kikubwa mno kwao kutokana na kuanza kazi hiyo ya uchimbaji muda mfupi uliopita na kuwa kiwango hicho kilipaswa kutolewa kwa wachimbaji wa muda mrefu.

Ngusaru alisema kwa wananchi wa vijiji vilivyopo jirani na mgodi huo sio rahisi kuelewa labda tu Mkurugenzi wa halmashauri hiyo aende kutoa elimu kwa wananchi hao ambapo aliomba jambo hilo lianghaliwe kwa jicho la karibu.

Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa TIC, Mhandisi Peter Chisawillo, aliupongeza uwekezaji wa mgodi huo ambao kazi nyingi zinafanywa na watanzania za kuendesha mitambo na teknolojia zingine hadi kupatikana kwa dhahabu na kueleza kuwa inaonesha thamani ya elimu walioipata na kuwa ni faida kwa nchi.

Dk.Mahenge akihitimisha ziara yake kwa kufanya kikao na wawekezaji wa Mkoa wa Singida alisema una fursa nyingi za uwekezaji na akaipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi kwa kuandaa mipango mizuri ya uwekezaji kwa kutenga maeneo na kupima ardhi ambapo aliziomba halmashauri zingine kuiga mfano huo.

Baadhi ya wawekezaji walioudhuria kikao hicho walieleza changamoto kadhaa walizonazo ni kuto thaminiwa na taasisi zingine kwa kurundikiwa kodi nyingi na kuorodheshewa  makosa ya kulipa faini ambapo waliomba wajengewe mazingira rafiki ili nao waweze kukua na kuwa wawekezaji wakubwa.

 

No comments:

Post a Comment