Na Dotto Mwaibale,
Singida
BOHARI ya Dawa (MSD)
imeanza kusambaza vyandarua zaidi ya 341,000 vyenye dawa katika shule za msingi
mkoani Singida kwa lengo la kutokomeza ugonjwa wa malaria ifikapo 2030.
Akizungumza wakati
wa uzinduzi wa kampeni ya ugawaji wa vyandarua katika shule za msingi mkoani
Singida, Meneja wa MSD Kanda ya Dodoma Mwanashehe Jumaa alisema kazi hiyo ya
usambaji wa vyandarua hivyo itafanyika kwa wiki tatu.
Alisema MSD ndio
yenye mamlaka ya kisheria ya
Kununua, Kuzalisha, Kuhifadhi na Kusambaza bidhaa za Afya hapa nchini ndio
maana wanafanya kazi hiyo.
Alisema MSD wanasambaza dawa, vifaa tiba na vitendanishi vya maabara na
kuwa vyandarua vinaingia kama vifaa tiba ambavyo vinatumika kumkingia mwananchi
asishambuliwe na malaria.
“MSD leo tupo mkoani Singida kushuhudia uzinduzi wa usamabazi wa
vyandarua zaidi ya 341,000 kwenye shule za msingi katika halmashauri za wilaya
sita isipokuwa moja ya Singida Manispaa na hilo ndilo jukumu tulilopewa na zoezi
hili la ugawaji wa vyandarua hivi tunatarajia kulifanya kwa kipindi cha wiki
tatu,” alisema Jumaa.
Alisema ili zoezi hilo liweze kukamilika wanahitaji kupata ushirikiano
kwa wadau wote ambao ni sehemu ya usambazi huo ambao ni wakuu wa wilaya,
wakurugenzi, maafisa elimu kuanzia mkoani hadi kwenye kata na wakuu wa shule na
kwa ushirikiano huo unaweza kuwafikisha kwenye lengo walilojiwekea.
Alisema MSD imepewa jukumu hilo kutokana na uzoefu mkubwa walionao na kuwa
na miundombinu ya usafirishaji ikiwemo ya kielektroniki kuanzia kuhifadhi hadi
usambazaji.
Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba ambaye alikuwa mgeni rasmi
akizindua kampeni hiyo alisema ugonjwa wa malaria bado ni tatizo mkoani hapa
kutokana na utafiti uliofanyika mwaka 2022 ulioonesha kiwango cha maambukizi ya
ugonjwa wa malaria kipo wastani wa asilimia 1.5 ikilinganishwa na kiwango cha
kitaifa ambacho ni asilimia 8.4 (TMIS 2022)
Alisema Halmashauri ya Itigi inakiwango kikubwa zaidi ya maambukizi ya
asilimia 9.8 ukilinganisha na Halmashauri ya Singida ambayo ina kiwango cha
chini zaidi ya asilimia 0.0 na kueleza kuwa Serikali bado inaendelea na juhudi
za kuhakikisha inatokomeza kabisa ugonjwa hatarai wa malaria kufikia 2030.
Mwakilishi wa Meneja Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Malaria kutoka Wizara
ya Afya , Theresia Shirima alisema adhima ya Serikali ni kuhakikisha hadi
ifikapo 2030 ugonjwa wa malaria unatokomezwa kabisa kwa kufanya usafi, kuharibu
mazalia ya mbu na njia nyingine ikiwamo ya ugawaji wa vyandarua mashuleni
ambapo wanafunzi watasaidia kuvifikisha kwenye kaya wanazotoka.
Alisema walengwa zaidi katika hizo kaya ni yale makundi ambayo yanakuwa
kwenye hatari ya kupata maambukizi ya ugonjwa huo ambao ni wajawazito na watoto
walio chini ya miaka mitano.
Afisa Elimu Mkoa wa Singida, Dkt. Elpidius Baganda alisema vyandarua
hivyo vinakwenda kugaiwa katika shule 670 na alitumia nafasi hiyo kuishukuru
Serikali chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuanzisha kampeni hiyo ambayo ni
muhimu kwa taifa.
No comments:
Post a Comment