Mkurugenzi Mtendaji wa TACAIDS Dkt. Leonard Maboko
.........................................................................
Na.
Aron Msigwa – MAELEZO.
07/9/2016.
Dar es salaam.
Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS) imewataka baadhi ya wadau, mashirika
na taasisi zilizo katika mapambano dhidi Ukimwi kuzingatia malengo ya awali ya
kuanzishwa kwa taasisi hizo na kuepuka
kuijiingiza katika shughuli za uanaharakati ambazo ni kinyume cha sheria.
Akizungumza katika kikao chake cha kwanza na wadau mbalimbali walio
katika mapambano dhidi ya Ukimwi leo jijini Dar es salaam, Mkurugenzi Mtendaji
wa TACAIDS Dkt. Leonard Maboko amesema kuwa baadhi ya wadau, mashirika na
taasisi zimekuwa zikifanya shughuli nje ya malengo ya awali ya kuanzishwa hali
inayosababisha mgongano katika jamii.
"Zipo baadhi ya taasisi zinazofanya shughuli nje ya malengo,
tunatambua Serikali haijakataa jitihada za makundi mbalimbali ya kupambana na
UKIMWI, sisi kama TACAIDS tutaendelea kuungana na Serikali kuhakikisha kuwa
zile taasisi zilizo kwenye mapambano zinasimamia malengo ya kuanzishwa kwake na
si vinginevyo" Amesisitiza Dkt.
Maboko.
Amewataka wadau na mashirika hayo kuendelea kujikita na kuongeza nguvu
katika utoaji wa elimu ,uhamasishaji wa wananchi kupima kwa hiari VVU kwa lengo
la kujua hali zao ili waweze kujikinga
na maambukizi mapya ya ugonjwa huo.
Pia amewata wadau hao kuangalia namna bora ya kuwafikia, kuwaelimisha na
kuwafuatilia wananchi walio katika makundi maalum kwenye mazingira hatarishi pia
kuongeza shughuli za utafiti zitakazoisaidia nchi kufikia lengo la maabukizi
sifuri.
Amesema
hali ya uelewa wa wananchi juu ugonjwa wa Ukimwi imefikia asilimia
90 kwa kuwa watanzania sasa wanauelewa kuhusu ugonjwa huo na hali zao . Aidha, wengi
wana uelewa iwapo wamepata maambukizi au la kutokana na kuongezeka kwa kampeni
za uhamasishaji na elimu ya kujikinga na maambukizi.
Kwa
upende wake Mkurugenzi wa Chama cha Uzazi na Malezi Bora Tanzania
(UMATI), Lulu Ng’wanakilala amesema Taasisi zinazosajiliwa kutoa huduma za
kuzuia na kupunguza maambukizi dhidi ya Ukimwi nchini Tanzania na kuanza
kujiingiza kwenye shughuli za uanaharakati zinakwamisha na kupunguza juhudi za
Serikali na wadau wengine wenye mapenzi mema walio kwenye mapambano dhidi ya
Ukimwi.
‘Sisi kama wadau wa hizi taasisi tunaongea lugha moja, NGOs
zinazosajiliwa kutoa huduma na kuanza kufanya uanaharakati kupitia masuala ya
Ukimwi zinakwenda kinyume cha maelengo,sisi tupo kwa lengo moja kuhakikisha
maambukizi yanafikia sifuri kwa kuhakikisha wote wanaotakiwa kupata huduma
wanafikiwa na huduma zetu hasa makundi yanayochangia kwa kiasi kikubwa
maambukizi ya Ukimwi’ Amesisitiza.
Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa Baraza
la Watu Wanaoishi na Virusi vya Ukimwi Tanzania (NACOFA) Bw. Deogratius Peter, akizungumzia
hatua ya baadhi ya taasisi kuenenda kinyume na malengo ya kuanzishwa kwake
amesema
‘Serikali imeshatoa Sera na miongozo mbalimbali inayosimamia shughuli za
utoaji wa huduma za mapambano dhidhi ya Ukimwi kwa taasisi, makundi na wadau
mbalimbali, Sisi pamoja na Serikali tunakubali
na kuheshimu juhudi za makundi haya katika mapambano dhidi ya Ukimwi, suala la uanaharakati
halikubaliki maadili lazima yazingatiwe katika utoaji wa huduma zetu tufuate
sheria za nchi ile kuepusha migongano isiyo ya lazima’ Amesisitiza.
Ameongeza kuwa taasisi zote zilizo katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa
Ukimwi lazima zikajikite katifa tafiti pia kuyafuatilia makundi yote yaliyo
katika mazingira hatarishi ambayo yanachangia kwa kiwango kikubwa kueneza maambukizi ya VVU.
