Subscribe Us

header ads

DMO na maofisa ushirika simamieni wana-AMCOS wajiunge na ushirka afya-Mwanri

NA TIGANYA VINCENT
RS TABORA
25 MAY 2018
MKUU wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri amewaagiza Waganga Wakuu wa Wilaya (DMO) na Maofisa Ushirika kushirikiana na viongozi wa  Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya ili kuhakikisha kuwa wanachama wote wa Vyama vya Ushirika vya Msingi(AMCOS) wanajiunga na Ushirika Afya ili waweze kuwa na afya nzuri wakati wote.
Hatua itawafanya kuwa na mazingira mazuri ya kupata matibabu ya aina yoyote hapa nchini jambo linalowafanya kuwa na uhakika wa uzalishaji mazao kwa wingi bila kuwa na kikwazo cha kupata tiba wakati wakiendelea na shughuli zao.
Mwanri alisema hayo jana wakati akiwa katika ziara yake kwenye Wilaya ya Igunga ya kuhamasisha wakulima wa pamba kujiunga na Bima ya Ushirika Afya na pia kupambana na utoro na mimba za utotoni.
Mkuu huyo wa Mkoa aliwataka Watendaji hao kuhakikisha wanakuwepo katika masoko yote ya mazao ya biashara ili kutoa elimu na hatimaye kuwasaidia kuwasajili wanachama wa AMCOS ambao watapenda kujiunga na Bima hiyo.
Alisema ni vema wananchi wajue kuwa mfumo wa Bima hiyo utamwezesha kutibiwa popote hapa nchini na kuondokana na matumizi ya fedha nyingi kutokana na kulipa fedha tasimu.
Mwanri alisema mtindo wa kisasa wa kuishi popote duniani ni kujiunga na Bima ya Afya kwa kuwa inasaidia kupunguza makali  ya matumizi ya fedha kwa ajili ya matibabu ya aina mbalimbali ambayo huzuka bila hodi wala kuja kuwa wakati yanakuja una fedha.
Kwa upande wa Meneja wa Mkoa wa Tabora wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Vedastus Kalungwani alisema kwa gharama ya shilingi 76,800/- mwanachama atapata matibabu ya aina yoyote katika vituo vya afya 6,000 nchini kote.
Alisema Bima hiyo itamwezesha mwanachama kupata matibabu kuanzia Zahanati hadi Hospitali ya Taifa kwa gharama hizo.
Naye Mwenyekiti wa Chaama Kikuu cha Ushirika cha Ingembensabo Lazaro Ngullo alisema kuwa huduma ya tiba anayopatiwa mwanachama wa Bima ya Afya ya aina yoyote inampa unafuu kuliko kama angetumia fedha tasilimu kupata matibabu ya aina ile ile.
Alisema Bima ya Afya inapunguza machungu ya gharama ambazo ungezitumia kama ungetoa fedha tasilimu na kuongeza kuwa ni vema wanaushirika wakachangamkia Bima ya Ushirika ili waweze kufaidi matunda ya jasho lao.

Ngullo alisema matatizo ya ugonjwa hayana hodi yanaweza kuzuka wakati wowote uwe na feda au hauna na hivyo ili kukabiliana nayo ni vema wanaushirika wakakata Bima ili kujiweka tayari wakati wowote.

Post a Comment

0 Comments