Random Posts

Afya za Watumishi Zizingatiwe ili Kuboresha Utendaji

 Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Anuai za Jamii, Ofisi ya Rais - Utumishi na Utawala Bora, Bi. Leila Mavika akisisitiza jambo katika kikao kazi cha Kamati Tendaji ya Kitaifa inayosimamia utekelezaji wa shughuli za VVU, UKIMWI   na Magonjwa Sugu Yasiyoambukizwa (MSY) mahala pa kazi mjini Morogoro.

Baadhi ya wajumbe wa Kamati Tendaji ya Kitaifa inayosimamia utekelezaji wa shughuli za VVU, UKIMWI   na Magonjwa Sugu Yasiyoambukizwa (MSY) mahala pa kazi wakiwa katika kikao kazi mjini Morogoro.


 TAARIFA KWA UMMA



AFYA ZA WATUMISHI ZIZINGATIWE ILI KUBORESHA UTENDAJI

Waajiri nchini wameelekezwa kuzingatia afya bora za watumishi katika taasisi zao kwani watumishi ndio nguvu kazi ambayo inawezesha shughuli kufanyika kwa ufasaha na kuleta tija kwa maendeleo ya taifa.

Hayo yamebainishwa na Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Anuai za Jamii, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Leila Mavika ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati Tendaji ya Kitaifa inayosimamia utekelezaji wa shughuli za VVU, UKIMWI   na Magonjwa Sugu Yasiyoambukizwa (MSY) mahala pa kazi wakati wa kikao kazi cha kamati hiyo mjini Morogoro.

Bi. Mavika amesema kuwa, kikao kazi hicho kimelenga kubadilishana taarifa, kutathmini hali halisi  ya utekelezaji  wa AFUA  za  UKIMWI  mahala pa kazi, pamoja na  kubuni mikakati itakayowezesha  Taasisi za Umma  kutekeleza  kisheria mwongozo na waraka unaohusu utoaji wa huduma kwa watumishi wanaoishi na VVU na UKIMWI  mahala pa kazi.

Bi. Mavika ameongeza kuwa, Serikali kupitia Ofisi ya Rais-Utumishi, imetoa miongozo mbalimbali ikiwemo Mwongozo wa Kudhibi VVU, UKIMWI na Magonjwa Sugu Yasiyoambukizwa mahala pa kazi katika Utumishi wa Umma wa mwaka 2014 unaoelekeza utaratibu na usimamizi wa masuala ya UKIMWI mahala pa kazi.

Aidha, Bi. Leila amesema, Serikali imetoa Waraka wa Utumishi Na. 2 wa mwaka 2014 kuhusu Kudhibiti Virusi vya UKIMWI, UKIMWI na Magonjwa Sugu Yasiyoambukizwa mahala pa kazi katika Utumishi wa Umma, waraka huo unawaelekeza waajiri namna ya kutoa huduma kwa watumishi wanaoishi na Virusi vya UKIMWI na UKIMWI.

Kwa Upande wake, Katibu wa Kamati hiyo Tendaji ya Kitaifa ambaye pia ni Afisa Mwitikio wa taasisi za Umma kutoka TACAIDS, Dkt. Ameir Hafidh amesema kuwa, jukumu lake kubwa ni kuhakikisha suala la UKIMWI sehemu za kazi katika sekta ya Umma linazingatiwa kwa mujibu wa Mwongozo na Waraka husika.

Dkt. Hafidh amesisitiza kuwa ni jukumu la mwajiri kuhakikisha anampatia huduma stahiki mtumishi anayeishi na Virusi vya UKIMWI na UKIMWI mara baada ya kujiweka wazi kwa mwajiri.

Wajumbe wa Kamati Tendaji Kitaifa wanaoshiriki katika kikao hicho ni kutoka Ofisi ya Rais-Utumishi, Tume ya Taifa ya Kudhibiti UKIMWI (TACAIDS), Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI, Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Tume ya Utumishi wa Umma Tanzania na Taasisi ya Chakula na Lishe.

IMETOLEWA NA:
KITENGO CHA MAWASILIANO SERIKALINI
OFISI YA RAIS (UTUMISHI)
 TAREHE 10 MEI, 2018

Post a Comment

0 Comments